We Love God!

God: "I looked for someone to take a stand for me, and stand in the gap" (Ezekiel 22:30)

Don't confuse God's patience with his final response

Bible – swahili_partial_NT – yohana

\h YOHANE

          INJILI KAMA ILIVYOANDIKWA NA
                 YOHANE

\c 1

Neno akawa Mtu

1 Hapo Mwanzo, Neno alikuwako; naye alikuwa na Mungu, naye alikuwa
Mungu.
2 Tangu mwanzo Neno alikuwa na Mungu.
3 Kwa njia yake vitu vyote viliumbwa; hakuna hata kiumbe kimoja
kilichoumbwa pasipo yeye.
4 Yeye alikuwa chanzo cha uhai na uhai huo ulikuwa mwanga wa watu.
5 Na mwanga huo huangaza gizani, nalo giza halikuweza kuushinda.

6 Mungu alimtuma mtu mmoja jina lake Yohane,
7 ambaye alikuja kuwaambia watu juu ya huo mwanga. Alikuja ili kwa
ujumbe wake watu wote wapate kuamini.
8 Yeye hakuwa huo mwanga, ila alikuja tu kuwaambia watu juu ya huo
mwanga.
9 Huu ndio mwanga halisi, mwanga unaokuja ulimwenguni, na
kuwaangazia watu wote.

10 Basi, Neno alikuwako ulimwenguni; na kwa njia yake ulimwengu
uliumbwa, lakini ulimwengu haukumtambua.
11 Alikuja katika nchi yake mwenyewe, nao walio wake hawakumpokea.
12 Lakini wale wote waliompokea na kumwamini, hao aliwapa uwezo wa
kuwa watoto wa Mungu.
13 Hawa wamekuwa watoto wa Mungu si kwa uwezo wa kibinadamu, wala
kwa nguvu za kimwili, wala kwa mapenzi ya mtu, bali Mungu mwenyewe ndiye
baba yao.

14 Naye Neno akawa mwanadamu, akakaa kwetu. Nasi tumeuona utukufu
wake, utukufu wake yeye aliye Mwana wa pekee wa Baba; amejaa neema na
ukweli.

15 Yohane aliwaambia watu habari zake, akasema kwa sauti, “Huyu
ndiye niliyemtaja wakati niliposema: <Anakuja mtu mmoja baada yangu
ambaye ni mkuu kuliko mimi, maana alikuwako kabla mimi sijazaliwa.”>

16 Kutokana na ukamilifu wake sisi tumepokea neema mfululizo.
17 Maana Mungu alitoa Sheria kwa njia ya Mose, lakini neema na kweli
vimekuja kwa njia ya Kristo.
18 Hakuna mtu aliyemwona Mungu wakati wowote ule. Mwana wa pekee
aliye sawa na Mungu ambaye ameungana na Baba, ndiye aliyetujulisha
habari za Mungu.

Ushahidi wa Yohane Mbatizaji
\r
\is (Mat. 3:1-12; Marko 1:1-8; Luka 3:1-18)
\ie

19 Huu ndio ushahidi Yohane alioutoa wakati viongozi wa Wayahudi
kule Yerusalemu walipowatuma makuhani wa Walawi kwake wamwulize: “Wewe
u nani?”
20 Yohane hakukataa kujibu swali hilo, bali alisema waziwazi, “Mimi
siye Kristo.”
21 Hapo wakamwuliza, “Basi, wewe ni nani? Je, wewe ni Eliya?”
Yohane akajibu, “La, mimi siye.” Wakamwuliza, “Je, wewe ni yule
nabii?” Yohane akawajibu, “La!”
22 Nao wakamwuliza, “Basi, wewe ni nani? Wasema nini juu yako
mwenyewe? Tuambie, ili tuwapelekee jibu wale waliotutuma.”
23 Yohane akawajibu, “Mimi ndiye yule ambaye nabii Isaya alisema
habari zake:

<Sauti ya mtu imesikika jangwani:
Nyoosheni njia ya Bwana.”>

24 Hao watu walikuwa wametumwa na Mafarisayo.
25 Basi, wakamwuliza Yohane, “Kama wewe si Kristo, wala Eliya, wala
yule nabii, mbona wabatiza?”
26 Yohane akawajibu, “Mimi nabatiza kwa maji, lakini yuko mmoja
kati yenu, msiyemjua bado.
27 Huyo anakuja baada yangu, lakini mimi sistahili hata kumfungua
kamba za viatu vyake.”

28 Mambo haya yalifanyika huko Bethania, ng’ambo ya mto Yordani
ambako Yohane alikuwa anabatiza.

Mwana-kondoo wa Mungu

29 Kesho yake, Yohane alimwona Yesu akimjia, akasema, “Huyu ndiye
Mwana-kondoo wa Mungu aondoaye dhambi ya ulimwengu!
30 Huyu ndiye niliyesema juu yake: <Baada yangu anakuja mtu mmoja
aliye mkuu zaidi kuliko mimi, maana alikuwako kabla mimi sijazaliwa!>
31 Mimi mwenyewe sikumfahamu, lakini nimekuja kubatiza kwa maji ili
watu wa Israeli wapate kumjua.”

32 Huu ndio ushahidi Yohane alioutoa: “Nilimwona Roho akishuka kama
njiwa kutoka mbinguni na kutua juu yake.
33 Mimi sikumjua, lakini yule aliyenituma nikabatize watu kwa maji
alikuwa ameniambia: <Mtu yule utakayemwona Roho akimshukia kutoka
mbinguni na kukaa juu yake, huyo ndiye anayebatiza kwa Roho Mtakatifu.>
34 Mimi nimeona na ninawaambieni kwamba huyu ndiye Mwana wa Mungu.”

Wanafunzi wa kwanza

35 Kesho yake, Yohane alikuwa tena mahali hapo pamoja na wanafunzi
wake wawili.
36 Alipomwona Yesu akipita akasema, “Tazameni! Huyu ndiye
Mwana-kondoo wa Mungu.”
37 Hao wanafunzi walimsikia Yohane akisema maneno hayo, wakamfuata
Yesu.
38 Basi, Yesu aligeuka, na alipowaona hao wanafunzi wanamfuata,
akawauliza, “Mnatafuta nini?” Nao wakamjibu, “Rabi (yaani Mwalimu),
unakaa wapi?”
39 Yesu akawaambia, “Njoni, nanyi mtaona.” Hao wanafunzi
wakamfuata, wakaona mahali alipokuwa anakaa, wakashinda naye siku hiyo.
Ilikuwa yapata saa kumi jioni.

40 Andrea, nduguye Simoni Petro, alikuwa mmoja wa hao wawili
waliokuwa wamemsikia Yohane akisema hivyo, wakamfuata Yesu.
41 Andrea alimkuta kwanza Simoni, ndugu yake, akamwambia,
“Tumemwona Masiha” (maana yake Kristo).
42 Kisha akampeleka Simoni kwa Yesu. Naye Yesu akamtazama Simoni
akasema, “Wewe ni Simoni mwana wa Yohane. Sasa utaitwa Kefa.” (maana
yake ni Petro, yaani, “Mwamba.”)

Filipo na Nathanieli wanaitwa

43 Kesho yake Yesu aliamua kwenda Galilaya. Basi, akamkuta Filipo,
akamwambia, “Nifuate.”
44 Filipo alikuwa mwenyeji wa Bethsaida, mji wa akina Andrea na
Petro.
45 Naye Filipo akamkuta Nathanieli, akamwambia, “Tumemwona yule
ambaye Mose aliandika juu yake katika kitabu cha Sheria, na ambaye
manabii waliandika habari zake, yaani Yesu Mwana wa Yosefu, kutoka
Nazareti.”
46 Naye Nathanieli akamwuliza Filipo, “Je, kitu chema chaweza
kutoka Nazareti?” Filipo akamwambia, “Njoo uone.”
47 Yesu alipomwona Nathanieli akimjia alisema juu yake, “Tazameni!
Huyo ni Mwisraeli halisi: hamna hila ndani yake.”
48 Naye Nathanieli akamwuliza, “Umepataje kunijua?” Yesu
akamwambia, “Ulipokuwa chini ya mtini hata kabla Filipo hajakuita,
nilikuona.”
49 Hapo Nathanieli akamwambia, “Mwalimu, wewe ni Mwana wa Mungu.
Wewe ni Mfalme wa Israeli!”
50 Yesu akamwambia, “Je, umeamini kwa kuwa nimekwambia kwamba
nilikuona chini ya mtini? Utaona makubwa zaidi kuliko haya.”
51 Yesu akaendelea kusema, “Nawaambieni kweli, mtaona mbingu
zinafunguka na malaika wa Mungu wakipanda na kushuka juu ya Mwana wa
Mtu.”

\c 2

Arusi mjini Kana

1 Siku ya tatu kulikuwa na arusi mjini Kana, mkoani Galilaya. Mama
yake Yesu alikuwapo,
2 naye Yesu alikuwa amealikwa arusini pamoja na wanafunzi wake.
3 Divai ilipokwisha, mama yake akamwambia, “Hawana divai!”
4 Yesu akamjibu, “Mama, usiniambie la kufanya. Saa yangu bado.”
5 Hapo mama yake akawaambia watumishi, “Lolote atakalowaambieni,
fanyeni.”

6 Hapo palikuwa na mitungi sita ya mawe, ambayo kila mmoja uliweza
kuchukua kiasi cha madebe mawili au matatu. Ilikuwa imewekwa hapo
kufuatana na desturi ya Kiyahudi ya kutawadha.
7 Yesu akawaambia, “Ijazeni mitungi hiyo maji.” Nao wakaijaza
mpaka juu.
8 Kisha akawaambia, “Sasa choteni mkampelekee mkuu wa karamu.”
9 Mkuu wa karamu alipoonja hayo maji, kumbe yalikuwa yamegeuka kuwa
divai. Yeye hakujua ilikotoka, (lakini wale watumishi waliochota maji
walijua). Mkuu wa karamu akamwita bwana arusi,
10 akamwambia, “Kila mtu huandaa divai nzuri kwanza hata wakisha
tosheka huandaa ile hafifu. Lakini wewe umeiweka divai nzuri mpaka
sasa!”

11 Yesu alifanya ishara hii ya kwanza huko Kana, Galilaya,
akaonyesha utukufu wake; nao wanafunzi wake wakamwamini.

12 Baada ya hayo, Yesu alishuka pamoja na mama yake, ndugu zake na
wanafunzi wake, wakaenda Kafarnaumu ambako walikaa kwa siku chache.

Yesu Hekaluni
\r
\is (Mat. 21:12-13; Marko 11:15-17; Luka 19:45-46)
\ie

13 Sikukuu ya Wayahudi ya Pasaka ilikuwa imekaribia; hivyo Yesu
akaenda Yerusalemu.
14 Hekaluni aliwakuta watu wakiuza ng’ombe, kondoo na njiwa, na
wavunja fedha walikuwa wamekaa kwenye meza zao.
15 Akatengeneza mjeledi wa kamba, akawafukuza wote nje ya Hekalu
pamoja na kondoo na ng’ombe wao, akazimwaga sarafu za wenye kuvunja
fedha na kupindua meza zao.
16 Akawaambia wale waliokuwa wanauza njiwa, “Ondoeni vitu hivi
hapa. Msiifanye nyumba ya Baba yangu kuwa soko!”
17 Wanafunzi wake wakakumbuka kwamba Maandiko yasema: “Upendo wangu
kwa nyumba yako waniua.”
\fr 2:17
\f Taz Zab 69:9

18 Baadhi ya Wayahudi wakamwuliza Yesu, “Utafanya muujiza gani
kuonyesha kwamba unayo haki kufanya mambo haya?”
19 Yesu akawaambia, “Vunjeni Hekalu hili, nami nitalijenga kwa siku
tatu.”
20 Hapo Wayahudi wakasema, “Hekalu hili lilijengwa kwa muda wa
miaka arobaini na sita. Je, wewe utalijenga kwa siku tatu?”

21 Lakini Yesu alikuwa anaongea juu ya Hekalu ambalo ni mwili wake.
22 Basi, alipofufuliwa kutoka wafu, wanafunzi wake walikumbuka
kwamba alikuwa amesema hayo, wakaamini Maandiko Matakatifu na yale
maneno aliyokuwa akisema Yesu.

Yesu ajua mioyo ya watu wote

23 Yesu alipokuwa Yerusalemu kwa sikukuu ya Pasaka, watu wengi
walimwamini walipoona ishara alizozifanya.
24 Lakini Yesu hakuwa na imani nao kwa sababu aliwajua wote.
25 Hakuhitaji kuambiwa chochote juu ya watu, maana aliyajua barabara
mambo yote yaliyomo mioyoni mwao.

\c 3

Yesu na Nikodemo

1 Kulikuwa na kiongozi mmoja Myahudi, wa kikundi cha Mafarisayo, jina
lake Nikodemo.
2 Siku moja alimwendea Yesu usiku, akamwambia, “Rabi, tunajua
kwamba wewe ni mwalimu uliyetumwa na Mungu, maana hakuna mtu awezaye
kufanya ishara unazozifanya Mungu asipokuwa pamoja naye.”

3 Yesu akamwambia, “Kweli nakwambia, mtu asipozaliwa upya hataweza
kuuona ufalme wa Mungu.”
4 Nikodemo akamwuliza, “Mtu mzima awezaje kuzaliwa tena? Hawezi
kuingia tumboni mwa mama yake na kuzaliwa mara ya pili!”
5 Yesu akamjibu, “Kweli nakwambia, mtu asipozaliwa kwa maji na
Roho, hawezi kamwe kuingia katika ufalme wa Mungu.
6 Mtu huzaliwa kimwili kwa baba na mama, lakini huzaliwa kiroho kwa
Roho.
7 Usistaajabu kwamba nimekwambia kuwa ni lazima kuzaliwa upya.
8 Upepo huvuma kuelekea upendako; waisikia sauti yake, lakini hujui
unakotoka wala unakokwenda. Ndivyo ilivyo kwa mtu aliyezaliwa kwa
Roho.”

9 Nikodemo akamwuliza, “Mambo haya yanawezekanaje?”
10 Yesu akamjibu, “Je, wewe ni mwalimu katika Israel na huyajui
mambo haya?
11 Kweli nakwambia, sisi twasema tunayoyajua na kushuhudia
tuliyoyaona, lakini ninyi hamkubali ujumbe wetu.
12 Ikiwa nimewaambieni mambo ya kidunia nanyi hamniamini, mtawezaje
kuamini nikiwaambieni mambo ya mbinguni?
13 Hakuna mtu aliyepata kwenda juu mbinguni isipokuwa Mwana wa Mtu
ambaye ameshuka kutoka mbinguni.

14 “Kama vile Mose alivyomwinua juu nyoka wa shaba kule jangwani,
naye Mwana wa Mtu atainuliwa juu vivyo hivyo,
15 ili kila anayemwamini awe na uzima wa milele.
16 Maana Mungu aliupenda ulimwengu hivi hata akamtoa Mwana wake wa
pekee, ili kila amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele.
17 Maana Mungu hakumtuma Mwanae ulimwenguni ili auhukumu ulimwengu,
bali aukomboe ulimwengu.

18 “Anayemwamini Mwana hahukumiwi; asiyemwamini amekwisha hukumiwa
kwa sababu hakumwamini Mwana wa pekee wa Mungu.
19 Na hukumu yenyewe ndiyo hii: Mwanga umekuja ulimwenguni lakini
watu wakapenda giza kuliko mwanga, kwani matendo yao ni maovu.
20 Kila mtu atendaye maovu anauchukia mwanga, wala haji kwenye
mwanga, maana hapendi matendo yake maovu yamulikwe.
21 Lakini mwenye kuuzingatia ukweli huja kwenye mwanga, ili matendo
yake yaonekane yametendwa kwa kumtii Mungu.”

Yesu na Yohane Mbatizaji

22 Baada ya hayo, Yesu alifika mkoani Yudea pamoja na wanafunzi
wake. Alikaa huko pamoja nao kwa muda, akibatiza watu.
23 Yohane pia alikuwa akibatiza watu huko Ainoni, karibu na Salemu,
maana huko kulikuwa na maji mengi. Watu walimwendea, naye akawabatiza.
(((
24 Wakati huo Yohane alikuwa bado hajafungwa gerezani.)

25 Ubishi ulitokea kati ya baadhi ya wanafunzi wa Yohane na Myahudi
mmoja kuhusu desturi za kutawadha.
26 Basi, wanafunzi hao wakamwendea Yohane na kumwambia, “Mwalimu,
yule mtu aliyekuwa pamoja nawe ng’ambo ya Yordani na ambaye wewe
ulimshuhudia, sasa naye anabatiza, na watu wote wanamwendea.”
27 Yohane akawaambia, “Mtu hawezi kuwa na kitu asipopewa na Mungu.
28 Nanyi wenyewe mwaweza kushuhudia kuwa nilisema: <Mimi siye
Kristo, lakini nimetumwa ili nimtangulie!>
29 Bibiarusi ni wake bwanaarusi, lakini rafiki yake bwana arusi,
anayesimama na kusikiliza, hufurahi sana anapomsikia bwana arusi
akisema. Ndivyo furaha yangu ilivyokamilishwa.
30 Ni lazima yeye azidi kuwa maarufu, na mimi nipungue.

Anayekuja kutoka mbinguni

31 “Anayekuja kutoka juu ni mkuu kuliko wote; atokaye duniani ni wa
dunia, na huongea mambo ya kidunia. Lakini anayekuja kutoka mbinguni ni
mkuu kuliko wote.
32 Yeye husema yale aliyoyaona na kuyasikia, lakini hakuna mtu
anayekubali ujumbe wake.
33 Lakini mtu yeyote anayekubali ujumbe wake anathibitisha kwamba
Mungu ni kweli.
34 Yule aliyetumwa na Mungu husema maneno ya Mungu, maana Mungu
humjalia mtu huyo Roho wake bila kipimo.
35 Baba anampenda Mwana na amemkabidhi vitu vyote.
36 Anayemwamini Mwana anao uzima wa milele; asiyemtii Mwana hatakuwa
na uzima wa milele, bali ghadhabu ya Mungu hubaki juu yake.”

\c 4

Yesu na mwanamke Msamaria

1 Mafarisayo walisikia kwamba Yesu alikuwa anabatiza na kuwapata
wanafunzi wengi kuliko Yohane. (((
2 Lakini ukweli ni kwamba Yesu hakuwa anabatiza ila wanafunzi wake.)
3 Basi, Yesu aliposikia hayo, alitoka Yudea akarudi Galilaya;
4 na katika safari hiyo ilimbidi apitie Samaria.

5 Basi, akafika Sukari, mji mmoja wa Samaria, karibu na shamba
ambalo Yakobo alikuwa amempa mwanawe, Yosefu.
6 Mahali hapo palikuwa na kisima cha Yakobo, naye Yesu, kutokana na
uchovu wa safari, akaketi kando ya kisima. Ilikuwa yapata saa sita
mchana.

7 Basi, mwanamke mmoja Msamaria akafika kuteka maji. Yesu
akamwambia, “Nipatie maji ninywe.”
\m
8 (Wakati huo wanafunzi wake walikuwa wamekwenda mjini kununua
chakula.)

9 Lakini huyo mwanamke akamwambia, “Wewe ni Myahudi; mimi ni
mwanamke Msamaria! Unawezaje kuniomba maji?” (Wayahudi hawakuwa na
ushirikiano na Wasamaria katika matumizi ya vitu.)
\m
10 Yesu akamjibu, “Kama tu ungalijua zawadi ya Mungu na ni nani
anayekwambia: <Nipatie maji ninywe,> ungalikwisha mwomba, naye angekupa
maji yaliyo hai.”

11 Huyo mama akasema, “Mheshimiwa, wewe huna chombo cha kutekea
maji, nacho kisima ni kirefu; utapata wapi maji yaliyo hai?
12 Au, labda wewe wajifanya mkuu kuliko babu yetu Yakobo? Yeye
alitupa sisi kisima hiki; na yeye mwenyewe, watoto wake na mifugo yake
walikunywa maji ya kisima hiki.”
13 Yesu akamjibu, “Kila anayekunywa maji haya ataona kiu tena.
14 Lakini atakayekunywa maji nitakayompa mimi, hataona kiu milele.
Maji nitakayompa yatakuwa ndani yake chemchemi ya maji ya uzima na
kumpatia uzima wa milele.”

15 Huyo mwanamke akamwambia, “Mheshimiwa, nipe maji hayo ili
nisione kiu tena; nisije tena mpaka hapa kuteka maji.”
16 Yesu akamwambia, “Nenda ukamwite mumeo uje naye hapa.”

17 Huyo mwanamke akamwambia, “Mimi sina mume.” Yesu akamwambia,
“Umesema kweli, kwamba huna mume.
18 Maana umekuwa na waume watano, na huyo unayeishi naye sasa si
mume wako. Hapo umesema kweli.”
19 Huyo Mwanamke akamwambia, “Mheshimiwa, naona ya kuwa wewe u
nabii.
20 Babu zetu waliabudu juu ya mlima huu, lakini ninyi mwasema kwamba
mahali pa kumwabudu Mungu ni kule Yerusalemu.”

21 Yesu akamwambia, “Niamini; wakati unakuja ambapo hamtamwabudu
Baba juu ya mlima huu, wala kule Yerusalemu.
22 Ninyi Wasamaria mnamwabudu yule msiyemjua, lakini sisi tunamjua
huyo tunayemwabudu, kwa maana wokovu unatoka kwa Wayahudi.
23 Lakini wakati unakuja, tena umekwisha fika, ambapo wanaoabudu
kweli, watamwabudu Baba kwa nguvu ya Roho; watu wanaomwabudu hivyo ndio
Baba anaotaka.
24 Mungu ni Roho, na watu wataweza tu kumwabudu kweli kwa nguvu ya
Roho wake.”
25 Huyo mama akamwambia, “Najua kwamba Masiha, aitwaye Kristo,
anakuja. Atakapokuja atatujulisha kila kitu.”
26 Yesu akamwambia, “Mimi ninayesema nawe, ndiye.”

27 Hapo wanafunzi wake wakarudi, wakastaajabu sana kuona anaongea na
mwanamke. Lakini hakuna mtu aliyesema: “Unataka nini?” au, “Kwa nini
unaongea na mwanamke?”

28 Huyo mama akauacha mtungi wake pale, akaenda mjini na kuwaambia
watu,
29 “Njoni mkamwone mtu aliyeniambia mambo yote niliyotenda! Je,
yawezekana kuwa yeye ndiye Kristo?”
30 Watu wakatoka mjini, wakamwendea Yesu.

31 Wakati huohuo wanafunzi wake walikuwa wanamsihi Yesu: “Mwalimu,
ule chakula.”
32 Lakini Yesu akawaambia, “Mimi ninacho chakula msichokijua
ninyi.”
33 Wanafunzi wake wakaulizana, “Je, kuna mtu aliyemletea chakula?”
34 Yesu akawaambia, “Chakula changu ni kufanya anachotaka yule
aliyenituma na kuitimiza kazi yake.
35 Ninyi mwasema: <Bado miezi minne tu, na wakati wa mavuno
utafika!> Lakini mimi nawaambieni, yatazameni mashamba; mazao yako
tayari kuvunwa.
36 Mvunaji anapata mshahara wake, na anakusanya mavuno kwa ajili ya
uzima wa milele; hivyo mpandaji na mvunaji watafurahi pamoja.
37 Kwa sababu hiyo msemo huu ni kweli: <Mmoja hupanda na mwingine
huvuna.>
38 Mimi nimewatuma mkavune mavuno ambayo hamkuyatolea jasho, wengine
walifanya kazi, lakini ninyi mnafaidika kutokana na jasho lao.”

39 Wasamaria wengi wa kijiji kile waliamini kwa sababu ya maneno
aliyosema huyo mama: “Ameniambia mambo yote niliyofanya.”
40 Wasamaria walimwendea Yesu wakamwomba akae nao; naye akakaa hapo
siku mbili.
41 Watu wengi zaidi walimwamini kwa sababu ya ujumbe wake.
42 Wakamwambia yule mama, “Sisi hatuamini tu kwa sababu ya maneno
yako; sisi wenyewe tumesikia, na tunajua kwamba huyu ndiye kweli Mwokozi
wa ulimwengu.”

Mwana wa ofisa anaponywa

43 Baada ya siku mbili Yesu aliondoka hapo, akaenda Galilaya.
44 Maana Yesu mwenyewe alisema waziwazi kwamba, “Nabii hapati
heshima katika nchi yake.”
45 Basi, alipofika Galilaya, Wagalilaya wengi walimkaribisha. Maana
nao pia walikuwa kwenye sikukuu ya Pasaka, wakayaona mambo yote Yesu
aliyotenda huko Yerusalemu wakati wa sikukuu hiyo.

46 Yesu alifika tena huko mjini Kana, mkoani Galilaya, mahali
alipogeuza maji kuwa divai. Kulikuwa na ofisa mmoja aliyekuwa na mtoto
mgonjwa huko Kafarnaumu.
47 Basi, huyo ofisa aliposikia kuwa Yesu alikuwa ametoka Yudea na
kufika Galilaya, alimwendea akamwomba aende kumponya mtoto wake
aliyekuwa mgonjwa mahututi.
48 Yesu akamwambia, “Msipoona ishara na maajabu hamtaamini!”
49 Huyo ofisa akamwambia, “Mheshimiwa, tafadhali twende kabla
mwanangu hajafa.”
50 Yesu akamwambia, “Nenda tu, mwanao yu mzima.” Huyo mtu akaamini
maneno ya Yesu, akaenda zake.
51 Alipokuwa bado njiani, watumishi wake walikutana naye,
wakamwambia kwamba mwanawe alikuwa mzima.
52 Naye akawauliza saa mtoto alipopata nafuu; nao wakamwambia,
“Jana saa saba mchana, homa ilimwacha.”
53 Huyo baba akakumbuka kwamba ilikuwa ni saa ileile ambapo Yesu
alimwambia: “Mwanao yu mzima.” Basi, yeye akaamini pamoja na jamaa
yake yote.
54 Hii ilikuwa ishara ya pili aliyoifanya Yesu alipokuwa anatoka
Yudea kwenda Galilaya.

\c 5

Yesu anaponya mtu karibu na bwawa la maji

1 Baada ya hayo kulikuwa na sikukuu ya Wayahudi, naye Yesu akaenda
Yerusalemu.
2 Huko Yerusalemu, karibu na mlango uitwao Mlango wa Kondoo,
kulikuwa na bwawa la maji liitwalo kwa Kiebrania Bethzatha, ambalo
lilikuwa na baraza tano zenye matao.
3 Humo barazani mlikuwa na wagonjwa wengi wamekaa: vipofu, viwete na
waliopooza.fa
4 missing
5 Basi, hapo palikuwa na mtu mmoja aliyekuwa mgonjwa kwa muda wa
miaka thelathini na minane.
6 Naye alipomwona huyo mtu amelala hapo, akatambua kwamba alikuwa
amekaa hapo kwa muda mrefu, akamwuliza, “Je, wataka kupona?”
7 Naye akajibu, “Mheshimiwa, mimi sina mtu wa kunipeleka majini
wakati yanapotibuliwa. Kila nikijaribu kuingia, mtu mwingine
hunitangulia.”
8 Yesu akamwambia, “Inuka, chukua mkeka wako utembee.”
9 Mara huyo mtu akapona, akachukua mkeka wake, akatembea. Jambo hili
lilifanyika siku ya Sabato.
10 Kwa hiyo baadhi ya Wayahudi wakamwambia huyo mtu aliyeponywa,
“Leo ni Sabato, si halali kubeba mkeka wako.”
\fm a
\fr 5:3b-4
\f Baadhi ya makala zina aya 3b-4: Walikuwa wakingojea maji yatibuliwe,
4 maana mara kwa mara malaika alishuka majini nyakati fulani na
kuyatibua. Mtu yeyote aliyekuwa wa kwanza kuingia majini baada ya maji
kutibuliwa, alipona ugonjwa wowote aliokuwa nao.

11 Lakini yeye akawaambia, “Yule mtu aliyeniponya ndiye
aliyeniambia: <Chukua mkeka wako, tembea.”>
12 Nao wakamwuliza, “Huyo mtu aliyekwambia: <Chukua mkeka wako,
tembea,> ni nani?”
13 Lakini yeye hakumjua huyo mtu aliyemponya, maana Yesu alikuwa
amekwisha ondoka mahali hapo, kwani palikuwa na umati mkubwa wa watu.
14 Basi, baadaye Yesu alimkuta huyo aliyeponywa Hekaluni,
akamwambia, “Sasa umepona; usitende dhambi tena, usije ukapatwa na
jambo baya zaidi.”
15 Huyo mtu akaenda, akawaambia viongozi wa Wayahudi kwamba Yesu
ndiye aliyemponya.

16 Kwa vile Yesu alifanya jambo hilo siku ya Sabato, Wayahudi
walianza kumdhulumu.
17 Basi, Yesu akawaambia, “Baba yangu anafanya kazi daima, nami pia
nafanya kazi.”

18 Kwa sababu ya maneno haya, viongozi wa Wayahudi walizidi kutafuta
njia ya kumwua Yesu: si kwa kuwa aliivunja Sheria ya Sabato tu, bali pia
kwa kuwa alisema kwamba Mungu ni Baba yake, na hivyo akajifanya sawa na
Mungu.

Mamlaka ya Mwana wa Mungu

19 Yesu akawaambia, “Kweli nawaambieni, Mwana hawezi kufanya kitu
peke yake; anaweza tu kufanya kile anachomwona Baba akikifanya. Maana
kile anachofanya Baba, Mwana hukifanya vilevile.
20 Baba ampenda Mwana, na humwonyesha kila kitu anachokifanya yeye
mwenyewe, tena atamwonyesha mambo makuu kuliko haya, nanyi mtastaajabu.
21 Kama vile Baba huwafufua wafu na kuwapa uzima, vivyo hivyo naye
Mwana huwapa uzima wale anaopenda.
22 Baba hamhukumu mtu yeyote; shughuli yote ya hukumu amemkabidhi
Mwana,
23 ili watu wote wamheshimu Mwana kama vile wanavyomheshimu Baba.
Asiyemheshimu Mwana hamheshimu Baba ambaye amemtuma.

24 “Kweli nawaambieni, anayesikia neno langu, na kumwamini yule
aliyenituma, anao uzima wa milele. Hatahukumiwa kamwe, bali amekwisha
pita kutoka kifo na kuingia katika uzima.
25 Kweli nawaambieni, wakati unakuja, tena umekwisha fika, ambapo
wafu wataisikia sauti ya Mwana wa Mungu, nao watakaoisikia, wataishi.
26 Kama vile Baba alivyo asili ya uhai, ndivyo pia alivyomjalia
Mwanawe kuwa asili ya uhai.
27 Tena amempa mamlaka ya kuhukumu kwa sababu yeye ni Mwana wa Mtu.
28 Msistaajabie jambo hili; maana wakati unakuja ambapo wote waliomo
makaburini wataisikia sauti yake,
29 nao watafufuka: wale waliotenda mema watafufuka na kuishi, na
wale waliotenda maovu watafufuka na kuhukumiwa.

Mashahidi wa Yesu

30 “Mimi siwezi kufanya kitu kwa uwezo wangu mwenyewe. Mimi nina
hukumu kama ninavyosikia kutoka kwa Baba, nayo hukumu yangu ni ya haki.
Nia yangu si kufanya nipendavyo mwenyewe, bali apendavyo yule
aliyenituma.
31 Nikijishuhudia mimi mwenyewe, ushahidi wangu hauwezi kukubaliwa
kuwa wa kweli.
32 Lakini yuko mwingine ambaye hutoa ushahidi juu yangu, nami najua
kwamba yote anayosema juu yangu ni ya kweli.
33 Ninyi mlituma ujumbe kwa Yohane naye aliushuhudia ukweli.
34 Si kwamba mimi nautegemea ushahidi wa wanadamu, lakini nasema
mambo haya ili mpate kuokolewa.
35 Yohane alikuwa kama taa iliyokuwa ikiwaka na kuangaza, nanyi
mlikuwa tayari kufurahia mwanga huo kwa kitambo.
36 Lakini mimi nina ushahidi juu yangu ambao ni mkuu zaidi kuliko
ule wa Yohane. Kwa maana kazi ninazofanya, kazi alizonipa Baba
nizifanye, ndizo zinazonishuhudia kwamba Baba ndiye aliyenituma.
37 Naye Baba aliyenituma hunishuhudia. Ninyi hamjapata kamwe kusikia
sauti yake, wala kuuona uso wake,
38 na ujumbe wake haukai ndani yenu maana hamkumwamini yule
aliyemtuma.
39 Ninyi huyachunguza Maandiko Matakatifu mkidhani kwamba ndani yake
mtapata uzima wa milele; na kumbe maandiko hayohayo yananishuhudia!
40 Hata hivyo, ninyi hamtaki kuja kwangu ili mpate uzima.
\il 5
ic
\is Kitabu cha Maandiko Matakatifu (Yoh 5:39)
\ie

41 “Shabaha yangu si kupata sifa kutoka kwa watu.
42 Lakini nawajua ninyi, najua kwamba upendo kwa Mungu haumo mioyoni
mwenu.
43 Mimi nimekuja kwa mamlaka ya Baba yangu, lakini hamnipokei; bali
mtu mwingine akija kwa mamlaka yake mwenyewe, mtampokea.
44 Mwawezaje kuamini, hali ninyi mnapenda kupokea sifa kutoka kwenu
ninyi wenyewe, wala hamtafuti sifa kutoka kwake yeye aliye peke yake
Mungu?
45 Msifikiri kwamba mimi nitawashtaki kwa Baba. Mose ambaye ninyi
mmemtumainia ndiye atakayewashtaki.
46 Kama kweli mngemwamini Mose, mngeniamini na mimi pia; maana Mose
aliandika juu yangu.
47 Lakini hamuyaamini yale aliyoandika, mtawezaje basi, kuamini
maneno yangu?”

\c 6

Yesu anawapa chakula watu elfu tano
\r
\is (Mat. 14:13-21; Marko 6:30-44; Luka 9:10-17)
\ie

1 Baada ya hayo, Yesu alivuka ziwa Galilaya (au Ziwa Tiberia).
2 Umati mkubwa wa watu ulimfuata kwa sababu watu hao walikuwa
wameona ishara alizokuwa akifanya kwa kuwaponya wagonjwa.
3 Yesu alipanda mlimani, akaketi pamoja na wanafunzi wake.
4 Sikukuu ya Wayahudi iitwayo Pasaka ilikuwa imekaribia.
5 Basi, Yesu na alipotazama na kuona umati wa watu ukija kwake,
alimwambia Filipo, “Tununue wapi mikate ili watu hawa wapate kula?”
(((
6 Alisema hivyo kwa kumjaribu Filipo, kwani alijua mwenyewe
atakalofanya.)
7 Filipo akamjibu, “Mikate ya denari mia mbili za fedha haiwatoshi
watu hawa hata kama ila mmoja atapata kipande kidogo tu!”
8 Mmoja wa wanafunzi wake aitwaye Andrea, nduguye Simoni Petro,
akamwambia,
9 “Yupo hapa mtoto mmoja aliye na mikate mitano ya shayiri na
samaki wawili; lakini hivi vyatosha nini kwa watu wengi kama hawa?”
10 Yesu akasema, “Waketisheni watu.” Palikuwa na nyasi tele mahali
hapo. Basi, watu wakaketi, jumla yapata wanaume elfu tano.
11 Yesu akaitwaa ile mikate, akamshukuru Mungu, akawagawia watu
waliokuwa wameketi; akafanya vivyo hivyo na wale samaki, kila mtu
akapata kadiri alivyotaka.
12 Watu waliposhiba Yesu akawaambia wanafunzi wake, “Kusanyeni
vipande vilivyobaki visipotee.”
13 Basi, wakakusanya vipande vya mikate ya shayiri walivyobakiza
wale watu waliokula, wakajaza vikapu kumi na viwili.
14 Watu walipoiona ishara hiyo aliyoifanya Yesu, wakasema, “Hakika
huyu ndiye nabii anayekuja ulimwenguni.”
15 Yesu akajua ya kuwa watu walitaka kumchukua wamfanye mfalme,
akaondoka tena, akaenda mlimani peke yake.
\il 5
ic
\is Denari (Yoh 6:7)
\ie

Yesu anatembea juu ya maji
\r
\is (Mat. 14:22-33; Marko 6:45-52)
\ie

16 Ilipokuwa jioni wanafunzi wake waliteremka hadi ziwani,
17 wakapanda mashua ili wavuke kwenda Kafarnaumu. Giza lilikuwa
limeingia, na Yesu alikuwa hajawafikia bado.
18 Ziwa likaanza kuchafuka kwa sababu upepo mkali ulikuwa unavuma.
19 Wanafunzi walipokuwa wamekwenda umbali wa kilomita tano au sita,
walimwona Yesu akitembea juu ya maji, anakaribia mashua; wakaogopa sana.
20 Yesu akawaambia, “Ni mimi, msiogope!”
21 Walifurahi kumchukua Yesu katika mashua; na mara mashua ikawasili
nchi kavu walipokuwa wanakwenda.

Watu wanamtafuta Yesu

22 Kesho yake umati wa watu wale waliobaki upande wa pili wa ziwa
walitambua kwamba kulikuwa na mashua moja tu pale, na Yesu hakuingia
katika mashua pamoja na wanafunzi wake, ila wanafunzi hao walikuwa
wamekwenda zao peke yao.
23 Mashua nyingine kutoka Tiberia zilifika mahali hapo watu
walipokula ile mikate, Bwana alipokwisha mshukuru Mungu.
24 Basi, hao watu walipogundua kwamba Yesu na wanafunzi wake
hawakuwapo mahali hapo, walipanda mashua, wakaenda Kafarnaumu
wakimtafuta.

Yesu mkate wa uzima

25 Wale watu walipomkuta Yesu ng’ambo ya pili wa ziwa walimwuliza,
“Mwalimu, ulifika lini hapa?”
26 Yesu akawajibu, “Kweli nawaambieni, mnanitafuta si kwa kuwa
mmeona ishara, bali kwa sababu mlikula ile mikate mkashiba.
27 Msikishughulikie chakula kiharibikacho; kishugulikieni chakula
kidumucho kwa ajili ya uzima wa milele. Mwana wa Mtu ambaye Baba
amemthibitisha atawapeni chakula hicho.”
28 Wao wakamwuliza, “Tufanye nini ili tuweze kuzitenda kazi za
Mungu?”
29 Yesu akawajibu, “Hii ndiyo kazi anayotaka Mungu muifanye:
kumwamini yule aliyemtuma.”
\fr 6:31
\f Taz Zab 78:24

30 Hapo wakamwambia, “Utafanya ishara gani ili tuione tupate
kukuamini? Utafanya kitu gani?
31 Wazee wetu walikula mana kule jangwani, kama yasemavyo Maandiko:
<Aliwalisha mkate kutoka mbinguni.”>
32 Yesu akawaambia, “Kweli nawaambieni, Mose hakuwapeni mkate
kutoka mbinguni; Baba yangu ndiye awapaye ninyi mkate halisi kutoka
mbinguni.
33 Maana mkate wa Mungu ni yule ashukaye kutoka mbinguni na aupaye
ulimwengu uzima.”
34 Basi, wakamwambia, “Mheshimiwa, tupe daima mkate huo.”
35 Yesu akawaambia, “Mimi ndimi mkate wa uzima. Anayekuja kwangu
hataona njaa; anayeniamini hataona kiu kamwe.
36 Lakini niliwaambieni kwamba ingawa mmeniona hamniamini.
37 Wote anaonipa Baba watakuja kwangu; nami sitamtupa nje yeyote
anayekuja kwangu,
38 kwani nimeshuka kutoka mbinguni si kwa ajili ya kufanya matakwa
yangu, ila kutimiza matakwa ya yule aliyenituma.
39 Na matakwa ya yule aliyenituma ndiyo haya: nisimpoteze hata mmoja
kati ya wale alionipa, ila niwafufue wote Siku ya mwisho.
40 Maana anachotaka Baba yangu ndicho hiki: kila amwonaye Mwana na
kumwamini awe na uzima wa milele; nami nitamfufua Siku ya mwisho.”

41 Basi, Wayahudi wakaanza kunung’unika kwa kuwa alisema: “Mimi ni
mkate ulioshuka kutoka mbinguni.”
42 Wakasema, “Je, huyu si mwana wa Yosefu? Tunawajua baba yake na
mama yake! Basi, anawezaje kusema kwamba ameshuka kutoka mbinguni?”
43 Yesu akawaambia, “Acheni kunung’unika ninyi kwa ninyi.
44 Hakuna mtu awezaye kuja kwangu, Baba aliyenituma asipomvuta
kwangu; nami nitamfufua mtu huyo Siku ya mwisho.
45 Manabii wameandika: <Watu wote watafundishwa na Mungu.> Kila mtu
anayemsikia Baba na kujifunza kutoka kwake, huja kwangu.
46 Hii haina maana kwamba yupo mtu aliyemwona Baba, isipokuwa yule
aliyetoka kwa Mungu; huyo ndiye aliyemwona Baba.
47 Kweli, nawaambieni, anayeamini anao uzima wa milele.
48 Mimi ni mkate wa uzima.
49 Wazee wenu walikula mana kule jangwani, lakini walikufa.
50 Huu ndio mkate kutoka mbinguni; mkate ambao anayekula hatakufa.
51 Mimi ni mkate hai ulioshuka kutoka mbinguni. Mtu yeyote akila
mkate huu ataishi milele. Na mkate nitakaompa ni mwili wangu ninaoutoa
kwa ajili ya uzima wa ulimwengu.”

52 Ndipo Wayahudi wakaanza kubishana kati yao:
53 Yesu akawaambia, “Kweli nawaambieni, msipokula mwili wa Mwana wa
Mtu na kunywa damu yake, hamtakuwa na uzima ndani yenu.
54 Anayekula mwili wangu na kunywa damu yangu anao uzima wa milele
nami nitamfufua siku ya mwisho.
55 Maana mwili wangu ni chakula cha kweli, na damu yangu ni kinywaji
cha kweli.
56 Aulaye mwili wangu na kunywa damu yangu, akaa ndani yangu, nami
nakaa ndani yake.
57 Baba aliye hai alinituma, nami naishi kwa sababu yake; vivyo
hivyo anilaye mimi ataishi pia kwa sababu yangu.
58 Basi, huu ndio mkate ulioshuka kutoka mbinguni; si kama mana
waliyokula babu zetu, wakafa. Aulaye mkate huu ataishi milele.”
59 Yesu alisema hayo alipokuwa akifundisha katika sunagogi kule
Kafarnaumu.

Maneno yaletayo uzima wa milele

60 Basi, wengi wa wafuasi wake waliposikia hayo, wakasema, “Haya ni
mambo magumu! Nani awezaye kuyasikiliza?”

61 Yesu alijua bila kuambiwa na mtu kwamba wanafunzi wake walikuwa
wananung’unika juu ya jambo hilo, akawauliza, “Je, jambo hili
linawafanya muwe na mashaka?
62 Itakuwaje basi, mtakapomwona Mwana wa Mtu akipanda kwenda kule
alikokuwa kwanza?
63 Roho ndiye atiaye uzima; binadamu peke yake hawezi. Maneno
niliyowaambieni ni Roho, ni uzima.
64 Hata hivyo, wako baadhi yenu wasioamini.” (Yesu alisema hivyo
kwani alijua tangu mwanzo ni kina nani wasioamini, na pia ni nani
atakayemsaliti.)
65 Kisha akasema, “Ndiyo maana niliwaambieni kwamba hakuna awezaye
kuja kwangu asipowezeshwa na Baba yangu.”

66 Kutokana na hayo, wengi wa wafuasi wake walirudi nyuma
wasiandamane naye tena.
67 Basi, Yesu akawauliza wale kumi na wawili, “Je, nanyi pia
mwataka kwenda zenu?”
68 Simoni Petro akamjibu, “Bwana, tutakwenda kwa nani? Wewe unayo
maneno yaletayo uzima wa milele.
69 Sisi tunaamini, na tunajua kwamba wewe ndiwe yule Mtakatifu wa
Mungu.”
70 Yesu akawaambia, “Je, sikuwachagua ninyi kumi na wawili? Hata
hivyo, mmoja wenu ni Ibilisi!”
71 Yesu alisema hayo juu ya Yuda, mwana wa Simoni Iskarioti; maana
huyu alikuwa ndiye atakayemsaliti, ingawa alikuwa mmoja wa wale kumi na
wawili.

\c 7

Yesu na ndugu zake

1 Baada ya hayo, Yesu alikuwa akitembea katika Galilaya. Hakutaka
kutembea mkoani Yudea kwa sababu viongozi wa Wayahudi walikuwa wanataka
kumwua.
2 Sikukuu ya Vibanda ya Wayahudi ilikuwa imekaribia.
3 Basi ndugu zake wakamwambia, “Ondoka hapa uende Yudea ili
wanafunzi wako wazione kazi unazozifanya.
4 Mtu hafanyi mambo kwa siri kama anataka kujulikana kwa watu.
Maadam unafanya mambo haya, basi, jidhihirishe kwa ulimwengu.” (((
5 Hata ndugu zake hawakumwamini!)
6 Basi, Yesu akawaambia, “Wakati wangu ufaao haujafika bado. Lakini
kwenu ninyi kila wakati unafaa.
7 Ulimwengu hauwezi kuwachukia ninyi, lakini mimi wanichukia kwa
sababu mimi nauambia wazi kwamba matendo yake ni maovu.
8 Ninyi nendeni kwenye sikukuu hiyo. Mimi siendi kwenye sikukuu
hiyo, maana saa yangu ifaayo haijafika.”
9 Alisema hayo kisha akabaki huko Galilaya.

Yesu kwenye sikukuu ya Vibanda

10 Baada ya ndugu zake kwenda kwenye sikukuu, Yesu naye alikwenda,
lakini hakuenda kwa hadhara bali kwa siri.
11 Viongozi wa Wayahudi walikuwa wanamtafuta kwenye sikukuu hiyo;
Wakauliza: “Yuko wapi?”

12 Kulikuwa na minong’ono mingi katika umati wa watu. Baadhi yao
walisema, “Ni mtu mwema.” Wengine walisema, “La! Anawapotosha watu.”
13 Hata hivyo hakuna mtu aliyethubutu kusema, habari zake hadharani
kwa kuwaogopa viongozi wa Wayahudi.

14 Sikukuu hiyo ilipofikia katikati, Yesu naye alikwenda Hekaluni,
akaanza kufundisha.
15 Basi, Wayahudi wakashangaa na kusema “Mtu huyu amepataje elimu
naye hakusoma shuleni?”
16 Hapo Yesu akawajibu, “Mafundisho ninayofundisha si yangu, bali
ni yake yeye aliyenituma.
17 Mtu anayependa kufanya yale anayotaka Mungu, atajua kama
mafundisho yangu yametoka kwa Mungu, au mimi najisemea tu mwenyewe.
18 Yeye anayejisemea tu mwenyewe anatafuta sifa yake mwenyewe;
lakini anayetafuta sifa ya yule aliyemtuma, huyo ni mwaminifu, na ndani
yake hamna uovu wowote.
19 Je, Mose hakuwapeni Sheria? Hata hivyo, hakuna hata mmoja wenu
anayeishika Sheria. Kwa nini mnataka kuniua?”
20 Hapo watu wakamjibu, “Una wazimu wewe! Nani anataka kukuua?”

21 Yesu akawajibu, “Kuna jambo moja nililofanya, nanyi
mnalistaajabia.
22 Mose aliwapeni ile desturi ya kutahiri. (Si kwamba desturi hiyo
ilitoka kwa Mose, bali ilitoka kwa mababu). Sasa ninyi humtahiri mtu
hata siku ya Sabato.
23 Ikiwa basi, mtu hutahiriwa hata siku ya Sabato kusudi Sheria ya
Mose isivunjwe, mbona mnanikasirikia kwa sababu nimemfanya mtu kuwa
mzima kabisa siku ya Sabato?
24 Msihukumu mambo kwa nje tu; toeni hukumu ya haki.”

Je, huyu ni Kristo?

25 Baadhi ya watu wa Yerusalemu walisema, “Je, yule mtu
wanayemtafuta wamuue si huyu?
26 Tazameni sasa! Anawaonya hadharani, wala hakuna mtu anayemwambia
hata neno. Je, yawezekana kuwa viongozi wametambua kweli kwamba huyu
ndiye Kristo?
27 Kristo atakapokuja hakuna mtu atakayejua mahali alikotoka, lakini
sisi tunajua alikotoka mtu huyu!”

28 Basi, Yesu alipokuwa anafundisha Hekaluni alipaaza sauti na
kusema, “Ati mnanijua; hata nilikotoka mnakujua! Hata hivyo, sikuja kwa
mamlaka yangu mwenyewe; ila yeye aliyenituma mimi ni wa kweli, nanyi
hamumjui.
29 Lakini mimi namjua kwa sababu nimetoka kwake, naye ndiye
aliyenituma.”

30 Basi, watu wakataka kumtia nguvuni, lakini hakuna mtu
aliyethubutu kumkamata kwa sababu saa yake ilikuwa haijafika bado.
31 Wengi katika ule umati wa watu walimwamini, wakasema, “Je,
Kristo akija atafanya ishara kubwa zaidi kuliko alizozifanya huyu?”

Walinzi wanatumwa kumkamata Yesu

32 Mafarisayo waliwasikia watu wakinong’ona maneno hayo juu ya Yesu.
Basi, wao pamoja na makuhani wakuu wakawatuma walinzi wamtie nguvuni.
33 Yesu akasema, “Bado niko nanyi kwa muda mfupi, kisha nitamwendea
yule aliyenituma.
34 Mtanitafuta lakini hamtaniona, maana pale nitakapokuwa ninyi
hamwezi kufika.”
35 Viongozi wa Wayahudi wakasema wao kwa wao, “Mtu huyu atakwenda
wapi ambapo hatutaweza kumpata? Atakwenda kwa Wayahudi waliotawanyika
kati ya Wagiriki, na kuwafundisha Wagiriki?
36 Ana maana gani anaposema: <Mtanitafuta lakini hamtanipata, na
mahali nitakapokuwa ninyi hamwezi kufika?”>

Mito ya maji yenye uzima

37 Siku ya mwisho ya sikukuu hiyo ilikuwa siku maalum. Yesu
alisimama, akasema kwa sauti kubwa, “Aliye na kiu na aje kwangu anywe.
38 Kama yasemavyo Maandiko Matakatifu: <Anayeniamini mimi, mito ya
maji yenye uzima itatiririka kutoka moyoni mwake!”> (((
39 Alisema hayo kumhusu Roho ambaye wale waliomwamini yeye
watampokea. Wakati huo Roho alikuwa hajafika kwa sababu Yesu alikuwa
hajatukuzwa bado.)

Mafarakano kati ya watu juu ya Yesu

40 Baadhi ya watu katika ule umati walisikia maneno hayo, wakasema,
“Kweli mtu huyu ndiye yule nabii!”
41 Wengine wakasema, “Huyu ndiye Kristo!” Lakini wengine walisema,
“Je, yawezekana Kristo akatoka Galilaya?
42 Maandiko Matakatifu yasemaje? Yanasema: <Kristo atatoka katika
ukoo wa Daudi, na atazaliwa Bethlehemu, mji wa Daudi!”>
43 Basi, kukatokea mafarakano juu yake katika ule umati wa watu.
44 Baadhi ya watu walitaka kumtia nguvuni lakini hakuna aliyejaribu
kumkamata.

Viongozi wa Wayahudi hawana imani

45 Kisha wale walinzi wakarudi kwa makuhani wakuu na Mafarisayo; nao
wakawauliza, “Kwa nini hamkumleta?”
46 Walinzi wakawajibu, “Hakuna mtu aliyepata kamwe kusema kama
asemavyo mtu huyu!”
47 Mafarisayo wakawauliza, “Je, nanyi pia mmedanganyika?
48 Je, mmekwisha mwona hata mmoja wa viongozi wa watu, au mmoja wa
Mafarisayo aliyemwamini?
49 Lakini umati huu haujui Sheria ya Mose; umelaaniwa!”

50 Mmoja wao alikuwa Nikodemo ambaye hapo awali alikuwa amemwendea
Yesu. Basi, yeye akawaambia,
51 “Je, Sheria yetu humhukumu mtu kabla ya kumsikia kwanza na kujua
anafanya nini?”
52 Nao wakamjibu, “Je, wewe pia umetoka Galilaya? Haya,
kayachunguze Maandiko Matakatifu nawe utaona kwamba Galilaya hakutoki
kamwe nabii!”

Mwanamke mzinzi
[[[
53 Basi, wote wakaondoka, kila mtu akaenda zake;

\c 8
1 lakini Yesu akaenda kwenye mlima wa Mizeituni.
2 Kesho yake asubuhi na mapema alikwenda tena Hekaluni. Watu wote
wakamwendea, naye akaketi akawa anawafundisha.
3 Basi, walimu wa Sheria na Mafarisayo wakamletea mwanamke mmoja
aliyefumaniwa katika uzinzi. Wakamsimamisha katikati yao.
4 Kisha wakamwuliza Yesu, “Mwalimu! Mwanamke huyu alifumaniwa
katika uzinzi.
5 Katika Sheria yetu Mose alituamuru mwanamke kama huyu apigwe mawe.
Basi, wewe wasemaje?”
6 Walisema hivyo kumjaribu, wapate kisa cha kumshtaki. Lakini Yesu
akainama chini, akaandika ardhini kwa kidole.
7 Walipozidi kumwuliza, Yesu akainuka, akawaambia, “Mtu asiye na
dhambi miongoni mwenu na awe wa kwanza kumpiga jiwe.”
8 Kisha akainama tena, akawa anaandika ardhini.
9 Waliposikia hivyo, wakaanza kutoweka mmojammoja, wakitanguliwa na
wazee. Yesu akabaki peke yake, na yule mwanamke amesimama palepale.
10 Yesu alipoinuka akamwuliza huyo mwanamke, “Wako wapi wale watu?
Je, hakuna hata mmoja aliyekuhukumu?”
11 Huyo mwanamke akamjibu, “Mheshimiwa, hakuna hata mmoja!” Naye
Yesu akamwambia, “Wala mimi sikuhukumu. Nenda zako; na tangu sasa
usitende dhambi tena.”]fb
\fm b
\fr 7:53-8:11
\f Makala nyingi za kale hazina sehemu hii, na baadhi ya tafsiri huiweka
mahali pengine.

Yesu mwanga wa ulimwengu

12 Yesu alipozungumza nao tena, aliwaambia, “Mimi ndimi mwanga wa
ulimwengu. Anayenifuata mimi hatembei kamwe gizani, bali atakuwa na
mwanga wa uzima.”

13 Basi, Mafarisayo wakamwambia, “Wewe unajishuhudia mwenyewe; kwa
hiyo ushahidi wako si halali.”
14 Yesu akawajibu, “Hata kama ninajishuhudia mwenyewe, ushahidi
wangu ni wa kweli kwa sababu mimi najua nilikotoka na ninakokwenda.
Lakini ninyi hamjui nilikotoka wala ninakokwenda.
15 Ninyi mnahukumu kwa fikira za kibinadamu, lakini mimi simhukumu
mtu.
16 Hata nikihukumu, hukumu yangu ni ya haki kwa sababu mimi siko
peke yangu; Baba aliyenituma yuko pamoja nami.
17 Imeandikwa katika Sheria yenu ya kwamba ushahidi wa watu wawili
ni halali.
18 Mimi najishuhudia mwenyewe, naye Baba aliyenituma, ananishuhudia
pia.”
19 Hapo wakamwuliza, “Baba yako yuko wapi?” Yesu akawajibu “Ninyi
hamnijui mimi wala hamumjui Baba. Kama mngenijua mimi, mngemjua na Baba
yangu pia.”

20 Yesu alisema maneno hayo kwenye chumba cha hazina alipokuwa
anafundisha Hekaluni. Wala hakuna mtu aliyemtia nguvuni, kwa sababu saa
yake ilikuwa haijafika bado.

Niendako ninyi hamwezi kufika

21 Yesu akawaambia tena, “Naenda zangu nanyi mtanitafuta, lakini
mtakufa katika dhambi zenu. Niendako mimi,ninyi hamwezi kufika.”
22 Basi, viongozi wa Wayahudi wakasema, “Je, atajiua? Mbona
anasema: <Niendako ninyi hamwezi kufika?”>
23 Yesu akawaambia, “Ninyi mmetoka papa hapa chini, mimi nimetoka
juu; ninyi ni wa ulimwengu huu, mimi si wa ulimwengu huu.
24 Ndiyo maana niliwaambieni mtakufa katika dhambi zenu. Kama
msipoamini kwamba <Mimi ndimi>, mtakufa katika dhambi zenu.”
25 Nao wakamwuliza, “Wewe ni nani?” Yesu akawajibu,
“Nimewaambieni tangu mwanzo!
26 Ninayo mengi ya kusema na kuhukumu juu yenu. Lakini yule
aliyenituma ni kweli; nami nauambia ulimwengu mambo yale tu
niliyoyasikia kutoka kwake.”

27 Hawakuelewa kwamba Yesu alikuwa akisema nao juu ya Baba.
28 Basi, Yesu akawaambia, “Mtakapokwisha mwinua Mwana wa Mtu hapo
ndipo mtakapojua kwamba <Mimi ndimi>, na kwamba sifanyi chochote mimi
mwenyewe, ila nasema tu yale Baba aliyonifundisha.
29 Yule aliyenituma yuko pamoja nami; yeye hakuniacha peke yangu
kwani nafanya daima yale yanayompendeza.”
30 Baada ya kusema hayo watu wengi walimwamini.

Ukweli utawapeni uhuru

31 Basi, Yesu akawaambia wale Wayahudi waliomwamini, “Kama
mkiyazingatia mafundisho yangu mtakuwa kweli wanafunzi wangu.
32 Mtaujua ukweli, nao ukweli utawapeni uhuru.”
33 Nao wakamjibu, “Sisi ni wazawa wa Abrahamu, na hatujapata kamwe
kuwa watumwa wa mtu yeyote yule. Una maana gani unaposema: <mtakuwa
huru?”>
34 Yesu akawajibu, “Kweli nawaambieni, kila mtu anayetenda dhambi
ni mtumwa wa dhambi.
35 Mtumwa hana makao ya kudumu nyumbani, lakini mwana anayo makao ya
kudumu.
36 Kama mwana akiwapeni uhuru mtakuwa huru kweli.
37 Najua kwamba ninyi ni wazawa wa Abrahamu. Hata hivyo, mnataka
kuniua kwa sababu hamuyakubali mafundisho yangu.
38 Mimi nasema yale aliyonionyesha Baba, lakini ninyi mwafanya yale
aliyowaambieni baba yenu.”

39 Wao wakamjibu, “Baba yetu ni Abrahamu!” Yesu akawaambia, “Kama
ninyi mngekuwa watoto wa Abrahamu, mngefanya kama alivyofanya Abrahamu,
40 Mimi nimewaambieni ukweli niliousikia kwa Mungu; hata hivyo,
ninyi mwataka kuniua. Abrahamu hakufanya hivyo!
41 Ninyi mnafanya mambo yaleyale aliyofanya babu yenu.” Wao
wakamwambia, “Sisi si watoto haramu! Tunaye baba mmoja tu, yaani
Mungu.”
42 Yesu akawaambia, “Kama Mungu angekuwa Baba yenu, mngenipenda
mimi, maana mimi nilitoka kwa Mungu na sasa niko hapa. Sikuja kwa
mamlaka yangu mwenyewe, ila yeye alinituma.
43 Kwa nini hamwelewi hayo ninayosema? Ni kwa kuwa hamwezi
kuusikiliza ujumbe wangu.
44 Ninyi ni watoto wa baba yenu Ibilisi na mnataka tu kutekeleza
tamaa za baba yenu. Yeye alikuwa muuaji tangu mwanzo; hana msimamo
katika ukweli, kwani ukweli haumo ndani yake. Kila asemapo uongo, husema
kutokana na hali yake ya maumbile, maana yeye ni mwongo na baba wa
uongo.
45 Mimi nasema ukweli, na ndiyo maana ninyi hamniamini.
46 Nani kati yenu awezaye kuthibitisha kuwa mimi nina dhambi? Ikiwa
basi nasema ukweli, kwa nini hamniamini?
47 Aliye wa Mungu husikiliza maneno ya Mungu. Lakini ninyi
hamsikilizi kwa sababu ninyi si (watu wa) Mungu.”

Yesu alikuwako kabla ya Abrahamu

48 Wayahudi wakamwambia, “Je, hatukusema kweli kwamba wewe ni
Msamaria, na tena una pepo?”
49 Yesu akajibu, “Mimi sina pepo; mimi namheshimu Baba yangu,
lakini ninyi hamniheshimu.
50 Mimi sijitafutii utukufu wangu mwenyewe; yuko mmoja mwenye
kuutafuta utukufu huo, naye ni hakimu.
51 Kweli nawaambieni, anayeuzingatia ujumbe wangu hatakufa milele.”
52 Basi, Wayahudi wakasema, “Sasa tunajua kweli kwamba wewe ni
mwendawazimu! Abrahamu alikufa, na manabii pia walikufa, nawe wasema
ati, <Anayeuzingatia ujumbe wangu hatakufa milele!>
53 Je, unajifanya mkuu zaidi kuliko baba yetu Abrahamu ambaye
alikufa? Hata na manabii walikufa. Wewe unajifanya kuwa nani?”
54 Yesu akawajibu, “Nikijitukuza mwenyewe, utukufu wangu si kitu.
Baba yangu ambaye ninyi mwasema ni Baba yenu, ndiye anayenitukuza.
55 Ninyi hamjapata kumjua, lakini mimi namjua. Na, nikisema simjui,
nitakuwa mwongo kama ninyi. Mimi namjua na ninashika neno lake.
56 Abrahamu, baba yenu, alishangilia aione siku yangu; naye aliiona,
akafurahi.”
57 Basi, Wayahudi wakamwambia, “Wewe hujatimiza miaka hamsini bado,
nawe umemwona Abrahamu?”
58 Yesu akawaambia, “Kweli nawaambieni, kabla Abrahamu hajazaliwa,
mimi niko.”
59 Hapo wakaokota mawe ili wamtupie, lakini Yesu akajificha, akatoka
Hekaluni.

\c 9

Yesu anamponya mtu aliyezaliwa kipofu

1 Yesu alipokuwa akipita alimwona mtu mmoja, kipofu tangu kuzaliwa.
2 Basi, wanafunzi wakamwuliza, “Mwalimu! Ni nani aliyetenda dhambi:
mtu huyu, ama wazazi wake, hata akazaliwa kipofu?”
3 Yesu akajibu, “Jambo hili halikutukia kwa sababu ya dhambi zake
yeye, wala dhambi za wazazi wake; ila alizaliwa kipofu ili nguvu ya
Mungu ionekane ikifanya kazi ndani yake.
4 Kukiwa bado mchana yatupasa kuendelea kufanya kazi za yule
aliyenituma; maana usiku unakuja ambapo mtu hawezi kufanya kazi.
5 Wakati ningali ulimwenguni, mimi ni mwanga wa ulimwengu.”
6 Baada ya kusema hayo, akatema mate chini, akafanyiza tope,
akampaka yule kipofu machoni,
7 akamwambia, “Nenda ukanawe katika bwawa la Siloamu.” (maana ya
jina hili ni “aliyetumwa”). Basi, huyo kipofu akaenda, akanawa, kisha
akarudi akiwa anaona.

8 Basi, jirani zake na wale waliokuwa wanajua kwamba hapo awali
alikuwa maskini mwombaji, wakasema, “Je, huyu siye yule maskini
aliyekuwa akiketi na kuomba?”
9 Baadhi yao wakasema, “Ndiye.” Wengine wakasema, “La! Ila
anafanana naye.” Lakini huyo aliyekuwa kipofu akasema, “Ni mimi!”
10 Basi, wakamwuliza, “Sasa, macho yako yalipataje kufumbuliwa?”
11 Naye akawajibu, “Yule mtu aitwaye Yesu alifanya tope, akanipaka
machoni na kuniambia: <Nenda ukanawe katika bwawa la Siloamu.> Basi,
mimi nikaenda, nikanawa, nikapata kuona.”
12 Wakamwuliza, “Yeye yuko wapi?” Naye akawajibu, “Mimi sijui!”

Uchunguzi kuhusu kuponywa kipofu

13 Kisha wakampeleka huyo mtu aliyekuwa kipofu kwa Mafarisayo.
14 Siku hiyo Yesu alipofanya tope na kumfumbua macho mtu huyo,
ilikuwa siku ya Sabato.
15 Basi, Mafarisayo wakamwuliza mtu huyo, “Umepataje kuona?” Naye
akawaambia, “Alinipaka tope machoni, nami nikanawa na sasa naona.”
16 Baadhi ya Mafarisayo wakasema, “Mtu huyu hakutoka kwa Mungu,
maana hashiki sheria ya Sabato.” Lakini wengine wakasema, “Mtu mwenye
dhambi awezaje kufanya ishara za namna hii?” Kukawa na mafarakano kati
yao.
17 Wakamwuliza tena huyo mtu aliyekuwa kipofu, “Maadam yeye
amekufungua macho, wasemaje juu yake?” Naye akawaambia, “Yeye ni
nabii!”

18 Viongozi wa Wayahudi hawakusadiki kwamba mtu huyo alikuwa kipofu
hapo awali na sasa anaona mpaka walipowaita wazazi wake.
19 Basi, wakawauliza hao wazazi, “Je, huyu ndiye mtoto wenu ambaye
ninyi mwasema alizaliwa kipofu? Sasa amepataje kuona?”
20 Wazazi wake wakajibu, “Tunajua kwamba huyu ni mtoto wetu, na
kwamba alizaliwa kipofu.
21 Lakini amepataje kuona, hatujui; na wala hatumjui yule
aliyemfumbua macho. Mwulizeni yeye mwenyewe; yeye ni mtu mzima, anaweza
kujitetea mwenyewe.”
22 Wazazi wake walisema hivyo kwa sababu waliwaogopa viongozi wa
Wayahudi kwani viongozi hao walikuwa wamepatana ya kwamba mtu yeyote
atakayekiri kwamba Yesu ni Kristo atafukuzwa nje ya sunagogi.
23 Ndiyo maana wazazi wake walisema: “Yeye ni mtu mzima,
mwulizeni.”

24 Basi, wakamwita tena aliyekuwa kipofu, wakamwambia, “Sema ukweli
mbele ya Mungu! Sisi tunajua kwamba mtu huyu ni mwenye dhambi.”
25 Yeye akajibu, “Kama ni mwenye dhambi mimi sijui. Lakini kitu
kimoja najua: Nilikuwa kipofu, na sasa naona.”
26 Basi, wakamwuliza, “Alikufanyia nini? Alikufumbuaje macho
yako?”
27 Huyo mtu akawajibu, “Nimekwisha waambieni, nanyi hamkusikiliza;
kwa nini mwataka kusikia tena? Je, ninyi pia mnataka kuwa wafuasi
wake?”
28 Lakini wao wakamtukana wakisema, “Wewe ni mfuasi wake; sisi ni
wafuasi wa Mose.
29 Sisi tunajua kwamba Mungu alisema na Mose, lakini mtu huyu
hatujui ametoka wapi!”
30 Naye akawajibu, “Hili ni jambo la kushangaza! Ninyi hamjui
ametoka wapi, lakini amenifumbua macho yangu!
31 Tunajua kwamba Mungu hawasikilizi watu wenye dhambi, ila
humsikiliza yeyote mwenye kumcha na kutimiza mapenzi yake.
32 Tangu mwanzo wa ulimwengu haijasikika kwamba mtu ameyafumbua
macho ya mtu aliyezaliwa kipofu.
33 Kama mtu huyu hakutoka kwa Mungu, hangeweza kufanya chochote!”
34 Wao wakamjibu, “Wewe ulizaliwa na kulelewa katika dhambi;
unawezaje kutufundisha sisi?” Basi, wakamfukuzia mbali.

Upofu wa roho

35 Yesu alisikia kwamba walikuwa wamemfukuzia mbali, naye alipomkuta
akamwuliza, “Je, wewe unamwamini Mwana wa Mtu?”
36 Huyo mtu akajibu, “Mheshimiwa, niambie yeye ni nani, ili nipate
kumwamini.”
37 Yesu akamwambia, “Umekwisha mwona, naye ndiye anayesema nawe
sasa.”
38 Basi, huyo mtu akasema, “Ninaamini Bwana!” Akamsujudia.

39 Yesu akasema, “Mimi nimekuja ulimwenguni kutoa hukumu, kusudi
wasioona wapate kuona, na wale wanaoona wawe vipofu.”
40 Baadhi ya Mafarisayo waliokuwa pamoja naye walisikia maneno hayo,
wakamwuliza, “Je, sisi pia ni vipofu?”
41 Yesu akawajibu, “Kama mngekuwa vipofu, hamngekuwa na hatia;
lakini sasa ninyi mwasema: <Sisi tunaona>, na hiyo yaonyesha kwamba mna
hatia bado.

\c 10

Mchungaji mwema

1 Yesu alisema “Kweli nawaambieni, yeyote yule asiyeingia katika
zizi la kondoo kwa kupitia mlangoni, bali hupenya na kuingia kwa njia
nyingine, huyo ni mwizi na mnyang’anyi.
2 Lakini anayeingia kwa kupitia mlangoni, huyo ndiye mchungaji wa
kondoo.
3 Mngoja mlango wa zizi humfungulia, na kondoo husikia sauti yake,
naye huwaita kondoo wake kila mmoja kwa jina lake na kuwaongoza nje.
4 Akisha watoa nje huwatangulia mbele nao kondoo humfuata, kwani
wanaijua sauti yake.
5 Kondoo hao hawawezi kumfuata mgeni, bali watamkimbia kwa sababu
hawaijui sauti yake.”
6 Yesu aliwaambia mfano huo, lakini wao hawakuelewa alichotaka
kuwaambia.

Yesu mchungaji mwema

7 Basi, akasema tena, “Kweli nawaambieni, mimi ni mlango wa kondoo.
8 Wale wengine wote waliokuja kabla yangu ni wezi na wanyang’anyi,
nao kondoo hawakuwasikiliza.
9 Mimi ni mlango. Anayeingia kwa kupitia kwangu ataokolewa; ataingia
na kutoka, na kupata malisho.
10 Mwizi huja kwa shabaha ya kuiba, kuua na kuharibu. Mimi nimekuja
mpate kuwa na uzima–uzima kamili.

11 “Mimi ni mchungaji mwema. Mchungaji mwema huutoa uhai wake kwa
ajili ya kondoo wake.
12 Mtu wa kuajiriwa ambaye si mchungaji, na wala kondoo si mali
yake, anapoona mbwa mwitu anakuja, huwaacha kondoo na kukimbia. Kisha
mbwa mwitu huwakamata na kuwatawanya.
13 Yeye hajali kitu juu ya kondoo kwa sababu yeye ni mtu wa mshahara
tu.
14 Mimi ni mchungaji mwema. Nawajua walio wangu, nao walio wangu
wananijua mimi,
15 kama vile Baba anijuavyo, nami nimjuavyo Baba. Mimi nayatoa
maisha yangu kwa ajili yao.
16 Tena ninao kondoo wengine ambao hawamo zizini humu. Inanibidi
kuwaleta hao pia, nao wataisikia sauti yangu, na kutakuwako kundi moja
na mchungaji mmoja.

17 “Baba ananipenda kwani nautoa uhai wangu ili nipate kuupokea
tena.
18 Hakuna mtu anayeninyang’anya uhai wangu; mimi na nautoa kwa hiari
yangu mwenyewe. Ninao uwezo wa kuutoa na uwezo wa kuuchukua tena. Hivi
ndivyo Baba alivyoniamuru nifanye.”

19 Kukawa tena na mafarakano kati ya Wayahudi kwa sababu ya maneno
haya.
20 Wengi wao wakasema, “Ana pepo; tena ni mwendawazimu! Ya nini
kumsikiliza?”
21 Wengine wakasema, “Haya si maneno ya mwenye pepo. Je, pepo
anaweza kuyafumbua macho ya vipofu?”

Yesu anakataliwa na Wayahudi
22 Huko Yerusalemu kulikuwa na sikukuu ya Kutabaruku. Wakati huo
ulikuwa wa baridi.
23 Naye Yesu akawa anatembea Hekaluni katika ukumbi wa Solomoni.
24 Basi, Wayahudi wakamzunguka, wakamwuliza, “Utatuacha katika
mashaka mpaka lini? Kama wewe ndiye Kristo, basi, tuambie wazi.”
25 Yesu akawajibu, “Nimewaambieni, lakini hamsadiki. Kazi
ninazozifanya mimi kwa jina la Baba yangu zinanishuhudia.
26 Lakini ninyi hamsadiki kwa sababu ninyi si kondoo wangu.
27 Kondoo wangu huisikia sauti yangu; mimi nawajua, nao hunifuata.
28 Mimi nawapa uzima wa milele; nao hawatapotea milele, wala hakuna
mtu atakayeweza kuwatoa mkononi mwangu.
29 Baba yangu ambaye ndiye aliyenipa hao ni mkuu kuliko wote, wale
hakuna awezaye kuwatoa mikononi mwake Baba.
30 Mimi na Baba, tu mmoja.”
\fr 10:34
\f Taz. Zab 82:6

31 Basi, Wayahudi wakachukua mawe ili wamtupie.
32 Yesu akawaambia, “Nimewaonyesheni kazi nyingi kutoka kwa Baba.
Ni ipi kati ya hizo inayowafanya mnipige mawe?”
33 Wayahudi wakamjibu, “Hatukupigi mawe kwa ajili ya tendo jema,
ila kwa sababu ya kukufuru! Maana wajifanya kuwa Mungu hali wewe ni
binadamu tu.”
34 Yesu akawajibu, “Je, haikuandikwa katika Sheria yenu: <Mimi
nimesema, ninyi ni miungu?>
35 Mungu aliwaita miungu wale waliopewa neno lake; nasi twajua
kwamba Maandiko Matakatifu yasema ukweli daima.
36 Je, yeye ambaye Baba alimweka wakfu na kumtuma ulimwenguni,
mnamwambia: <Unakufuru>, eti kwa sababu nilisema: <Mimi ni Mwana wa
Mungu?>
37 Kama sifanyi kazi za Baba yangu msiniamini.
38 Lakini ikiwa ninazifanya, hata kama hamniamini, walau ziaminini
hizo kazi mpate kujua na kutambua kwamba Baba yuko ndani yangu, nami
niko ndani yake.”
39 Wakajaribu tena kumkamata lakini akachopoka mikononi mwao.

40 Yesu akaenda tena ng’ambo ya mto Yordani, mahali Yohane alipokuwa
akibatiza, akakaa huko.
41 Watu wengi walimwendea wakasema, “Yohane hakufanya ishara
yoyote. Lakini yale yote Yohane aliyosema juu ya mtu huyu ni kweli
kabisa.”
42 Watu wengi mahali hapo wakamwamini.

\c 11

Kifo cha Lazaro

1 Mtu mmoja aitwaye Lazaro, mwenyeji wa Bethania, alikuwa mgonjwa.
(Kijiji cha Bethania kilikuwa mahali walipokaa Maria na Martha, dada
yake.
2 Maria ndiye yule aliyempaka Bwana marashi na kumpangusa kwa nywele
zake. Lazaro, kaka yake, ndiye aliyekuwa mgonjwa.)
3 Basi, hao dada wakatuma ujumbe huu kwa Yesu: “Bwana, rafiki yako
ni mgonjwa!”

4 Yesu aliposikia hivyo akasema, “Ugonjwa huo hautaleta kifo, ila
ni kwa ajili ya kumtukuza Mungu; ameugua ili kwa njia hiyo Mwana wa
Mungu atukuzwe.”

5 Yesu aliwapenda Martha, dada yake na Lazaro.
6 Alipopata habari kwamba Lazaro ni mgonjwa, Yesu aliendelea kukaa
mahali hapo alipokuwa kwa siku mbili zaidi.
7 Kisha akawaambia wanafunzi wake, “Twendeni tena Yudea!”
8 Wanafunzi wakamwambia, “Mwalimu! Muda mfupi tu umepita tangu
Wayahudi walipotaka kukuua kwa mawe, nawe unataka kwenda huko tena?”
9 Yesu akajibu, “Je, saa za mchana si kumi na mbili? Basi, mtu
akitembea mchana hawezi kujikwaa kwa kuwa anauona mwanga wa ulimwengu
huu.
10 Lakini mtu akitembea usiku atajikwaa kwa maana mwanga haumo ndani
yake.”
11 Yesu alipomaliza kusema maneno hayo, akawaambia, “Rafiki yetu
Lazaro amelala, lakini mimi nitakwenda kumwamsha.”
12 Wanafunzi wake wakamwambia, “Bwana, ikiwa amelala, basi
atapona.”
13 Wao walidhani kwamba alikuwa amesema juu ya kulala usingizi,
kumbe alikuwa amesema juu ya kifo cha Lazaro.
14 Basi, Yesu akawaambia waziwazi, “Lazaro amekufa;
15 Lakini nafurahi kwa ajili yenu kwamba sikuwako huko, ili mpate
kuamini. Haya, twendeni kwake.”
16 Thoma (aitwaye Pacha) akawaambia wanafunzi wenzake, “Twendeni
nasi tukafe pamoja naye!”

Yesu ni ufufuo na uzima

17 Yesu alipofika huko alikuta Lazaro amekwisha kaa kaburini kwa
siku nne.
18 Kijiji cha Bethania kilikuwa karibu na Yerusalemu umbali upatao
kilomita tatu.
19 Wayahudi wengi walikuwa wamefika kwa Martha na Maria kuwafariji
kwa kifo cha kaka yao.

20 Basi, Martha aliposikia kwamba Yesu alikuwa anakuja, akaenda
kumlaki; lakini Maria alibaki nyumbani.
21 Martha akamwambia Yesu, “Bwana, kama ungalikuwa hapa, kaka yangu
hangalikufa!
22 Lakini najua kwamba hata sasa chochote utakachomwomba Mungu,
atakupa.”
23 Yesu akamwambia, “Kaka yako atafufuka.”
24 Martha akamjibu, “Najua kwamba atafufuka wakati wa ufufuo, siku
ya mwisho.”
25 Yesu akamwambia, “Mimi ndimi ufufuo na uzima. Anayeniamini mimi
hata kama anakufa, ataishi:
26 na kila anayeishi na kuniamini, hatakufa kamwe. Je, waamini
hayo?”
27 Martha akamwambia, “Ndiyo Bwana! Naamini kwamba wewe ndiwe
Kristo, Mwana wa Mungu, yule ajaye ulimwenguni.”

Yesu analia machozi

28 Baada ya kusema hayo, Martha alikwenda kumwita Maria, dada yake,
akamwabia faraghani, “Mwalimu yuko hapa, anakuita.”
29 Naye aliposikia hivyo, akainuka mara, akamwendea Yesu.
30 Yesu alikuwa hajaingia kijijini, ila alikuwa bado mahali palepale
Martha alipomlaki.
31 Basi, Wayahudi waliokuwa nyumbani pamoja na Maria wakimfariji
walipomwona ameinuka na kutoka nje ghafla, walimfuata. Walidhani alikuwa
anakwenda kaburini kuomboleza.

32 Basi, Maria alipofika mahali pale Yesu alipokuwa na kumwona,
alipiga magoti, akamwabia, “Bwana, kama ungalikuwa hapa, kaka yangu
hangalikufa!”
33 Yesu alipomwona analia, na wale Wayahudi waliokuja pamoja naye
wanalia pia, alijawa na huzuni na kufadhaika moyoni.
34 Kisha akawauliza, “Mlimweka wapi?” Wakamwambia, “Bwana, njoo
uone.”
35 Yesu akalia machozi.
36 Basi, Wayahudi wakasema, “Tazameni jinsi alivyompenda!”
37 Lakini baadhi yao wakasema, “Je, huyu aliyemfumbua macho yule
kipofu, hakuweza kumfanya Lazaro asife?”

Yesu anamfufua Lazaro

38 Basi, Yesu akiwa amehuzunika tena moyoni, akafika kaburini.
Kaburi lenyewe lilikuwa pango, na lilikuwa limefunikwa kwa jiwe.
39 Yesu akasema, “Ondoeni hilo jiwe!” Martha, dada yake huyo
aliyekufa, akamwambia, “Bwana, amekwishaanza kunuka; amekaa kaburini
siku nne!”
40 Yesu akamwambia, “Je, sikukwambia kwamba ukiamini utaona utukufu
wa Mungu?”
41 Basi, wakaliondoa lile jiwe. Yesu akatazama juu mbinguni,
akasema, “Nakushukuru Baba kwa kuwa wewe wanisikiliza.
42 Najua kwamba unanisikiliza daima. Lakini nimesema hayo kwa ajili
ya watu hawa waliopo hapa ili wapate kuamini kwamba wewe ndiwe
uliyenituma.”
43 Alipokwisha sema hayo, akaita kwa sauti kubwa: “Lazaro! Toka
nje!”
44 Huyo aliyekuwa amekufa akatoka nje, huku amefungwa sanda miguu na
mikono, na uso wake umefunikwa. Yesu akawaambia, “Mfungueni, mkamwache
aende zake.”

Njama za kumwua Yesu
\r
\is (Mat. 26:1-5; Marko 14:1-2; Luka 22:1-2)
\ie

45 Basi, Wayahudi wengi waliokuwa wamefika kwa Maria walipoona
kitendo hicho alichokifanya Yesu wakamwamini.
46 Lakini baadhi yao walikwenda kwa Mafarisayo wakatoa taarifa ya
jambo hilo alilofanya Yesu.
47 kwa hiyo makuhani wakuu na Mafarisayo wakafanya kikao cha Baraza
kuu, wakasema, “Tufanye nini? Mtu huyu anafanya ishara nyingi mno.
48 Tukimwacha tu watu wote watamwamini, nao Waroma watakuja
kuliharibu Hekalu letu na taifa letu!”
49 Hapo, mmoja wao aitwaye Kayafa, ambaye alikuwa Kuhani Mkuu mwaka
huo, akawaambia, “Ninyi hamjui kitu!
50 Je, hamwoni kwamba ni afadhali kwenu mtu mmoja afe kwa ajili ya
watu, kuliko taifa zima liangamizwe?”
51 Yeye hakusema hivyo kwa hiari yake mwenyewe, bali kwa vile
alikuwa Kuhani Mkuu mwaka huo, alibashiri kwamba Yesu atakufa kwa ajili
ya taifa lao;
52 na wala si kwa ajili yao tu, bali pia apate kuwaleta pamoja
watoto wa Mungu waliotawanyika.

53 Basi, tangu siku hiyo viongozi wa Wayahudi walifanya mipango ya
kumwua Yesu.
54 Kwa hiyo, Yesu hakutembea tena hadharani kati ya Wayahudi, bali
alitoka hapo, akaenda mahali karibu na jangwa, katika mji uitwao
Efraimu. Akakaa huko pamoja na wanafunzi wake.
55 Sikukuu ya Wayahudi ya Pasaka ilikuwa karibu, na watu wengi
walikwenda Yerusalemu ili wajitakase kabla ya sikukuu hiyo.
56 Basi, wakawa wanamtafuta Yesu; nao walipokusanyika pamoja
Hekaluni wakaulizana, “Mwaonaje? Yaonekana kwamba haji kabisa kwenye
sikukuu, au sivyo?”
57 Makuhani wakuu na Mafarisayo walikuwa wametoa amri kwamba mtu
akijua mahali aliko Yesu awaarifu kusudi wamtie nguvuni.

\c 12

Yesu anapakwa mafuta
\r
\is (Mat. 26:6-13; Marko 14:3-9)
\ie

1 Siku sita kabla ya sikukuu ya Pasaka, Yesu alifika Bethania
alikoishi Lazaro ambaye Yesu alikuwa amemfufua kutoka wafu.
2 Huko walimwandalia chakula cha jioni, naye Martha akawa
anawatumikia. Lazaro alikuwa mmoja wa wale waliokuwa mezani pamoja na
Yesu.
3 Basi, Maria alichukua chupa ya marashi ya nardo safi ya thamani
kubwa, akampaka Yesu miguu na kuipangusa kwa nywele zake. Nyumba yote
ikajaa harufu ya marashi.
4 Basi, Yuda Iskarioti, mmoja wa wale kumi na wawili ambaye ndiye
atakayemsaliti Yesu, akasema,
5 “Kwa nini marashi hayo hayakuuzwa kwa fedha dinari mia tatu,
wakapewa maskini?”
6 Alisema hivyo, si kwa kuwa alijali chochote juu ya maskini, bali
kwa sababu alikuwa mweka hazina, na kwa kuwa alikuwa mwizi, mara kwa
mara aliiba kutoka katika hiyo hazina.
7 Lakini Yesu akasema, “Msimsumbue huyu mama! Mwacheni ayaweke kwa
ajili ya siku ya mazishi yangu.
8 Maskini mtakuwa nao siku zote, lakini hamtakuwa nami siku zote.”
\il 5
ic
\is Nardo (Yoh 12:3)
\ie

Njama za kumwua Lazaro

9 Wayahudi wengi walisikia kwamba Yesu alikuwa Bethania. Basi,
wakafika huko si tu kwa ajili ya kumwona Yesu, ila pia wapate kumwona
Lazaro ambaye Yesu alimfufua kutoka wafu.
10 Makuhani wakuu waliamua pia kumwua Lazaro,
11 Maana kwa sababu ya Lazaro Wayahudi wengi waliwaasi viongozi wao,
wakamwamini Yesu.

Yesu anaingia Yerusalemu kwa shangwe
\r
\is (Mat. 21:1-11; Marko 11:1-11; Luka 19:28-40)
\ie

12 Kesho yake, kundi kubwa la watu waliokuja kwenye sikukuu
walisikia kuwa Yesu alikuwa njiani kuja Yerusalemu.
13 Basi, wakachukua matawi ya mitende, wakatoka kwenda kumlaki;
wakapaaza sauti wakisema: “Hosana! Abarikiwe huyo ajaye kwa jina la
Bwana. Abarikiwe mfalme wa Israeli.”
\fr 12:13
\f Taz Zab 118:25,26

14 Yesu akampata mwana punda mmoja akapanda juu yake kama yasemavyo
Maandiko:

15 “Usiogope mji wa Sioni!

Tazama, Mfalme wako anakuja,
Amepanda mwana punda.”
\m
16 Wakati huo wanafunzi wake hawakuelewa mambo hayo, lakini Yesu
alipokwisha tukuzwa, ndipo walipokumbuka kwamba hayo yalikuwa
yameandikwa juu yake, na kwamba watu walikuwa wamemtendea hivyo.

17 Kundi la watu wale waliokuwa pamoja naye wakati alipomwita Lazaro
kutoka kaburini, akamfufua kutoka wafu, walisema yaliyotukia.
18 Kwa hiyo umati huo wa watu ulimlaki, maana wote walisikia kwamba
Yesu alikuwa amefanya ishara hiyo.
19 Basi, Mafarisayo wakaambiana, “Mnaona? Hatuwezi kufanya
chochote! Tazameni, ulimwengu wote unamfuata.”

Wagiriki kadhaa wanataka kumwona Yesu

20 Kulikuwa na Wagiriki kadhaa miongoni mwa watu waliokuwa wamefika
Yerusalemu kuabudu wakati wa sikukuu hiyo.
21 Hao walimwendea Filipo, mwenyeji wa Bethsaida katika Galilaya,
wakasema, “Mheshimiwa, tunataka kumwona Yesu.”
22 Filipo akaenda akamwambia Andrea, nao wawili wakaenda kumwambia
Yesu.
23 Yesu akawaambia, “Saa ya kutukuzwa kwa Mwana wa Mtu imefika!
24 Kweli nawaambieni, punje ya ngano hubaki punje tu isipokuwa
ikianguka katika udongo na kufa. Kama ikifa, basi huzaa matunda mengi.
25 Anayependa maisha yake, atayapoteza; anayeyachukia maisha yake
katika ulimwengu huu, atayaweka kwa ajili ya uzima wa milele.
26 Anayetaka kunitumikia ni lazima anifuate, hivyo kwamba popote
pale nilipo mimi ndipo na mtumishi wangu atakapokuwa. Mtu yeyote
anayenitumikia Baba yangu atampa heshima.

Yesu anasema juu ya kifo chake

27 “Sasa roho yangu imefadhaika, na niseme nini? Je, niseme: <Baba,
usiruhusu saa hii inifikie>? Lakini ndiyo maana nimekuja–ili nipite
katika saa hii.
28 Baba, ulitukuze jina lako.” Hapo sauti ikasema kutoka mbinguni,
“Nimelitukuza, na nitalitukuza tena.”

29 Umati wa watu waliokuwa wamesimama hapo walisikia sauti hiyo, na
baadhi yao walisema, “Malaika ameongea naye!”
30 Lakini Yesu akawaambia, “Sauti hiyo haikutokea kwa ajili yangu
mimi, ila kwa ajili yenu.
31 Sasa ndio wakati wa ulimwengu huu kuhukumiwa; sasa mtawala wa
ulimwengu huu atapinduliwa.
32 Nami nitakapoinuliwa juu ya nchi nitamvuta kila mmoja kwangu.”
(((
33 Kwa kusema hivyo alionyesha atakufa kifo gani).

34 Basi, umati huo ukamjibu, “Sisi tunaambiwa na Sheria yetu kwamba
Kristo atadumu milele. Wawezaje basi, kusema ati Mwana wa Mtu anapaswa
kuinuliwa? Huyo Mwana wa Mtu ni nani?”
35 Yesu akawaambia, “Mwanga bado uko nanyi kwa muda mfupi. Tembeeni
mngali mnao huo mwanga ili giza lisiwapate; maana atembeaye gizani hajui
aendako.
36 Basi, wakati mnao huo mwanga uaminini ili mpate kuwa watu wa
mwanga.” Baada ya kusema maneno hayo, Yesu alikwenda zake na kujificha
mbali nao.
\fr 12:34
\f Taz Zab 110:4

Watu hawana imani

37 Ingawa Yesu alifanya miujiza hii yote mbele yao, wao
hawakumwamini.
38 Hivyo maneno aliyosema nabii Isaya yakatimia:

“Bwana, nani aliyeuamini ujumbe wetu?
Na uwezo wa Bwana umedhihirishwa kwa nani?”

39 Hivyo hawakuweza kuamini, kwani Isaya tena alisema:

40 “Mungu ameyapofusha macho yao,

amezipumbaza akili zao;
wasione kwa macho yao,
wasielewe kwa akili zao;
wala wasinigeukie, asema Bwana,
ili nipate kuwaponya.”

41 Isaya alisema maneno haya kwa sababu aliuona utukufu wa Yesu,
akasema habari zake.

42 Hata hivyo, wengi wa viongozi wa Wayahudi walimwamini Yesu.
Lakini kwa sababu ya Mafarisayo, hawakumkiri hadharani kwa kuogopa
kwamba watatengwa na sunagogi.
43 Walipendelea kusifiwa na watu kuliko kusifiwa na Mungu

Neno la Yesu linahukumu

44 Kisha Yesu akasema kwa sauti kubwa, “Mtu aliyeniamini, haniamini
mimi tu, ila anamwamini pia yule aliyenituma.
45 Anayeniona mimi anamwona pia yule aliyenituma.
46 Mimi ni mwanga, nami nimekuja ulimwenguni ili wote wanaoniamini
wasibaki gizani.
47 Anayeyasikia maneno yangu lakini hayashiki mimi sitamhukumu;
maana sikuja kuhukumu ulimwengu bali kuuokoa.
48 Asiyeyashika maneno yangu anaye wa kumhukumu: neno lile
nililosema ni hakimu wake siku ya mwisho.
49 Mimi sikunena kwa mamlaka yangu mwenyewe, ila Baba aliyenituma
ndiye aliyeniamuru niseme nini na niongee nini.
50 Nami najua kuwa amri yake huleta uzima wa milele. Basi, mimi
nasema tu yale Baba aliyoniagiza niyaseme.”

\c 13

Yesu anawaosha mitume miguu

1 Ilikuwa kabla ya sikukuu ya Pasaka. Yesu alijua kwamba saa yake ya
kuondoka ulimwenguni na kwenda kwa Baba ilikuwa imefika. Alikuwa
amewapenda daima watu wake walioko duniani; naam, aliwapenda mpaka
mwisho!

2 Basi, Yesu na wanafunzi wake walikuwa mezani kwa chakula cha
jioni. Ibilisi alikwisha mtia Yuda, mwana wa Simoni Iskarioti, nia ya
kumsaliti Yesu.
3 Yesu alijua kwamba Baba alikuwa amemkabidhi kila kitu, na kwamba
alikuwa ametoka kwa Mungu na anarudi kwa Mungu.
4 Basi, Yesu aliondoka mezani, akaweka kando vazi lake, akachukua
kitambaa na kujifunga kiunoni.
5 Kisha akatia maji katika bakuli, akaanza kuwaosha wanafunzi wake
miguu na kuipangusa kwa kile kitambaa alichojifungia.
6 Basi, akamfikia Simoni Petro; naye Petro akasema, “Bwana, wewe
utaniosha miguu mimi?”
7 Yesu akamjibu, “Huelewi sasa ninachofanya lakini utaelewa
baadaye.”
8 Petro akamwambia, “Wewe hutaniosha miguu kamwe!” Yesu akamjibu,
“Nisipokuosha hutakuwa na uhusiano nami tena.”
9 Simoni Petro akamwambia, “Bwana, nioshe, si miguu tu, bali na
mikono yangu na kichwa pia.”
10 Yesu akamwambia, “Aliyekwisha oga hana lazima ya kunawa
isipokuwa miguu, maana amekwisha takata mwili wote. Ninyi mmetakata,
lakini si nyote.” (((
11 Yesu alimjua yule ambaye atamsaliti, ndiyo maana alisema: “Ninyi
mmetakata, lakini si nyote.”)

12 Alipokwisha waosha miguu na kuvaa tena vazi lake, aliketi mezani,
akawaambia, “Je, mmeelewa hayo niliyowatendeeni?
13 Ninyi mwaniita Mwalimu na Bwana, nanyi mwasema vyema, kwa kuwa
ndimi.
14 Basi, ikiwa mimi niliye Bwana na Mwalimu, nimewaosha ninyi miguu,
nanyi pia mnapaswa kuoshana miguu.
15 Nimewapeni mfano, ili nanyi pia mfanye kama nilivyowafanyieni.
16 Kweli nawaambieni, mtumishi si mkuu zaidi kuliko bwana wake, wala
mtume si mkuu zaidi kuliko yule aliyemtuma.
17 Basi, ikiwa mwayajua hayo, mtakuwa na heri mkiyatekeleza.

18 “Haya nisemayo hayawahusu ninyi nyote. Mimi nawajua wale
niliowachagua. Lakini lazima yatimie Maandiko Matakatifu yasemayo: <Yule
aliyeshiriki chakula changu amegeuka kunishambulia.>
19 Mimi nimewaambieni mambo haya sasa kabla hayajatokea, ili
yatakapotokea mpate kuamini kuwa mimi ndimi.
20 Kweli nawaambieni anayempokea yule ninayemtuma anaponipokea mimi;
na anayenipokea mimi, anampokea yule aliyenituma.”
\fr 13:18
\f Taz Zab 41:9

Yesu anabashiri kwamba atasalitiwa
\r
\is (Mat. 26:20-25; Marko 14:17-21; Luka 22:21-23)
\ie

21 Alipokwisha sema hayo, Yesu alifadhaika sana rohoni, akasema
wazi, “Kweli nawaambieni, mmoja wenu atanisaliti!”
22 Wanafunzi wakatazama wasiweze kabisa kujua anasema nani.
23 Mmoja wa wanafunzi, ambaye Yesu alikuwa anampenda sana, alikuwa
ameketi karibu na Yesu.
24 Basi, Simoni Petro akamwashiria na kusema: “Mwulize anasema juu
ya nani.”
25 Mwanafunzi huyo akasogea karibu zaidi na Yesu, akamwuliza,
“Bwana, ni nani?”
26 Yesu akajibu, “Yule nitakayempa kipande cha mkate nilichochovya
katika sahani, ndiye.” Basi, akatwaa kipande cha mkate, akakichovya
katika sahani, akampa Yuda, mwana wa Simoni Iskarioti.
27 Yuda alipokwisha pokea kipande hicho, Shetani akamwingia. Basi
Yesu akamwambia, “Unachotaka kufanya, kifanye haraka!”
28 Lakini hakuna hata mmoja wa wale waliokaa pale mezani aliyefahamu
kwa nini alikuwa amemwambia hivyo.
29 Kwa kuwa Yuda alikuwa na wajibu wa kuutunza mfuko wa fedha,
baadhi yao walidhani kwamba Yesu alikuwa amemwambia anunue
vilivyohitajiwa kwa sikukuu, au kwamba alikuwa amemwambia akatoe
chochote kwa maskini.
30 Basi, Yuda alipokwisha twaa kile kipande cha mkate, akatoka nje
mara. Na ilikuwa usiku.

Amri mpya

31 Baada ya Yuda kuondoka, Yesu akasema, “Sasa Mwana wa Mtu
ametukuzwa, naye Mungu ametukuzwa ndani yake.
32 Na kama utukufu wa Mungu umefunuliwa ndani ya Mwana, basi, naye
Mungu ataudhihirisha utukufu wa Mwana ndani yake mwenyewe, na atafanya
hivyo mara.

33 “Watoto wangu, bado niko nanyi kwa muda mfupi tu. Mtanitafuta,
lakini sasa nawaambieni yale niliyowaambia viongozi wa Wayahudi:
<Niendako ninyi hamwezi kwenda!>
34 Nawapeni amri mpya: pendaneni; pendaneni kama nilivyowapenda
ninyi.
35 Mkipendana, watu wote watajua kwamba ninyi ni wanafunzi wangu.”

Yesu anabashiri kuwa Petro atamkana
\r
\is (Mat. 26:31-35; Marko 14:27-31; Luka 22:31-34)
\ie

36 Simoni Petro akamwuliza, “Bwana, unakwenda wapi?” Yesu akajibu,
“Niendako huwezi kunifuata sasa, lakini utanifuata baadaye.”
37 Petro akamwambia “Bwana, kwa nini siwezi kukufuata sasa? Niko
tayari kufa kwa ajili yako!”
38 Yesu akajibu, “Je, uko tayari kweli kufa kwa ajili yangu? Kweli
nakwambia, kabla jogoo hajawika utanikana mara tatu!”

\c 14

Yesu njia ya kwenda kwa Baba

1 Yesu aliwaambia, “Msifadhaike mioyoni mwenu. Mwaminini Mungu,
niaminini na mimi pia.
2 Nyumbani mwa Baba yangu mna makao mengi; la sivyo ningalikwisha
waambieni. Sasa nakwenda kuwatayarishieni nafasi.
3 Na nikienda na kuwatayarishieni nafasi, nitarudi na kuwachukueni
kwangu, ili nanyi muwe pale nilipo mimi.
4 Mnajua njia ya kwenda huko ninakokwenda.”

5 Thoma akamwuliza, “Bwana, hatujui unakokwenda, tutawezaje basi,
kuijua hiyo njia?”
6 Yesu akamjibu, “Mimi ni njia, na ukweli na uzima. Hakuna awezaye
kwenda kwa Baba ila kwa kupitia kwangu.
7 Ikiwa mnanijua mimi mnamjua na Baba yangu pia. Na tangu sasa,
mnamjua, tena mmekwisha mwona.”

8 Filipo akamwambia, “Bwana, tuonyeshe Baba, nasi tutatosheka.”
9 Yesu akamwambia, “Filipo, nimekaa nanyi muda wote huu, nawe
hujanijua? Aliyekwisha niona mimi amemwona Baba. Unawezaje basi, kusema:
<Tuonyeshe Baba?>
10 Je, huamini kwamba mimi niko ndani ya Baba, naye Baba yuko ndani
yangu? Maneno ninayowaambieni nyote siyasemi kwa mamlaka yangu; Baba
aliye ndani yangu anafanya kazi yake.
11 Mnapaswa kuniamini ninaposema kwamba mimi niko ndani ya Baba naye
Baba yuko ndani yangu. Ama sivyo, aminini kwa sababu ya mambo
ninayofanya.
12 Kweli nawaambieni, anayeniamini atafanya mambo ninayofanya mimi;
naam, atafanya hata makuu zaidi, maana nakwenda kwa Baba.
13 Na chochote mtakachoomba kwa jina langu nitafanya, ili Baba
atukuzwe ndani ya Mwana.
14 Mkiniomba chochote kwa jina langu, nitawafanyieni.

Roho Mtakatifu

15 “Mkinipenda mtazishika amri zangu.
16 Nami nitamwomba Baba naye atawapeni Msaidizi mwingine, atakayekaa
nanyi milele.
17 Yeye ni Roho wa kweli. Ulimwengu hauwezi kumpokea kwa sababu
hauwezi kumwona wala kumjua. Lakini ninyi mnamjua kwa sababu anabaki
nanyi na yu ndani yenu.

18 “Sitawaacha ninyi yatima; nitakuja tena kwenu.
19 Bado kidogo nao ulimwengu hautaniona tena, lakini ninyi mtaniona;
na kwa kuwa mimi ni hai, nanyi pia mtakuwa hai.
20 Siku ile itakapofika mtajua kwamba mimi niko ndani ya Baba, nanyi
mko ndani yangu, nami ndani yenu.
21 Azipokeaye amri zangu na kuzishika, yeye ndiye anipendaye. Naye
anipendaye mimi atapendwa na Baba yangu, nami nitampenda na
kujidhihirisha kwake.”

22 Yuda (si yule Iskarioti) akamwambia, “Bwana, itawezekanaje wewe
kujidhihirisha kwetu na si kwa ulimwengu?”
23 Yesu akamjibu, “Mtu akinipenda atashika neno langu, na Baba
yangu atampenda, nasi tutakuja kwake na kukaa naye.
24 Asiyenipenda hashiki maneno yangu. Na neno mlilosikia si langu,
bali ni lake Baba aliyenituma.

25 “Nimewaambieni mambo haya nikiwa bado pamoja nanyi
26 lakini Msaidizi, Roho Mtakatifu, ambaye Baba atamtuma kwa jina
langu, atawafundisheni kila kitu na kuwakumbusheni yote niliyowaambieni.

27 “Nawaachieni amani; nawapeni amani yangu. Siwapi ninyi kama vile
ulimwengu ufanyavyo. Msiwe na wasiwasi, wala msifadhaike.
28 Mlikwisha sikia nikiwaambieni: <Ninakwenda zangu, kisha nitarudi
tena kwenu.> Kama mngalinipenda mngalifurahi kwa sababu ninakwenda kwa
Baba, maana yeye ni mkuu kuliko mimi.
29 Nimewaambieni haya sasa kabla hayajatokea, ili yatakapotokea
mpate kuamini.
30 Sitasema nanyi tena mambo mengi, maana mtawala wa ulimwengu huu
anakuja. Kwangu mimi hawezi kitu;
31 lakini ulimwengu unapaswa kujua kwamba nampenda Baba, na ndiyo
maana nafanya kila kitu kama Baba alivyoniamuru. Simameni, tutoke
hapa!”

\c 15

Yesu mzabibu wa kweli

1 “Mimi ni mzabibu wa kweli, na Baba yangu ndiye mkulima.
2 Yeye huliondoa ndani yangu kila tawi lisilozaa matunda, na kila
tawi lizaalo hulisafisha lipate kuzaa zaidi.
3 Ninyi mmekwisha kuwa safi kwa sababu ya ule ujumbe niliowaambieni.
4 Kaeni ndani yangu, nami nikae ndani yenu. Tawi haliwezi peke yake
kuzaa matunda lisipokaa katika mzabibu hali kadhalika nanyi hamwezi
kuzaa matunda msipokaa ndani yangu.
\il 5
ic
\is Mzabibu (Yoh 15:1)
\ie

5 “Mimi ni mzabibu, nanyi ni matawi yake. Akaaye ndani yangu, nami
ndani yake, huyo atazaa matunda mengi, maana bila mimi hamwezi kufanya
chochote.
6 Mtu yeyote asipokaa ndani yangu hutupwa nje kama tawi litupwalo
nje hata likakauka. Watu huliokota tawi la namna hiyo na kulitupa motoni
liungue.
7 Mkikaa ndani yangu na maneno yangu yakikaa ndani yenu, basi,
ombeni chochote mtakacho nanyi mtapewa.
8 Baba yangu hutukuzwa kama mkizaa matunda mengi na kuwa wanafunzi
wangu.
9 Mimi nimewapenda ninyi kama vile Baba alivyonipenda mimi. Kaeni
katika pendo langu.
10 Mkizishika amri zangu mtakaa katika pendo langu, kama vile nami
nilivyozishika amri za Baba yangu na kukaa katika pendo lake.
11 Nimewaambieni mambo haya ili furaha yangu ikae ndani yenu, na
furaha yenu ikamilike.
12 Hii ndiyo amri yangu: pendaneni; pendaneni kama nilivyowapenda
ninyi.
13 Hakuna upendo mkuu zaidi kuliko upendo wa mtu atoaye uhai wake
kwa ajili ya rafiki zake.
14 Ninyi ni rafiki zangu mkifanya ninayowaamuru.
15 Ninyi siwaiti tena watumishi, maana mtumishi hajui anachofanya
bwana wake. Lakini mimi nimewaita ninyi rafiki, kwa sababu nimewajulisha
yote ambayo nimeyasikia kutoka kwa Baba yangu.
16 Ninyi hamkunichagua mimi; mimi niliwachagueni na kuwatuma mwende
mkazae matunda, matunda yadumuyo, naye Baba apate kuwapa ninyi chochote
mumwombacho kwa jina langu.
17 Basi, amri yangu kwenu ndiyo hii: pendaneni.

Chuki ya ulimwengu

18 “Kama ulimwengu ukiwachukia ninyi, kumbukeni kwamba umenichukia
mimi kabla haujawachukia ninyi.
19 Kama mngalikuwa watu wa ulimwengu, ulimwengu ungaliwapenda ninyi
kama watu wake. Lakini kwa vile ninyi si wa ulimwengu, ila mimi
nimewachagueni kutoka ulimwenguni, kwa sababu hiyo ulimwengu
unawachukieni.
20 Kumbukeni niliyowaambieni: mtumishi si mkuu zaidi kuliko bwana
wake. Ikiwa wamenitesa mimi, watawatesa na ninyi pia; kama wameshika
neno langu, watalishika na lenu pia.
21 Lakini hayo yote watawatendeeni ninyi kwa sababu ya jina langu,
kwani hawamjui yeye aliyenituma.
22 Kama nisingalikuja na kusema nao wasingalikuwa na hatia; lakini
sasa hawawezi kujitetea kwamba hawana dhambi.
23 Anayenichukia mimi, anamchukia na Baba yangu pia.
24 Kama nisingalifanya kwao mambo ambayo hakuna mtu mwingine
amekwisha yafanya wasingalikuwa na hatia; lakini sasa wameona
niliyoyafanya wakinichukia mimi, wakamchukia na Baba yangu pia.
25 Na hivi ni lazima yatimie yale yaliyoandikwa katika Sheria yao:
<Wamenichukia bure!>

26 “Atakapokuja huyo Msaidizi nitakayemtuma kwenu kutoka kwa Baba,
huyo Roho wa kweli atokaye kwa Baba, yeye atanishuhudia mimi.
27 Nanyi pia mtanishuhudia kwa kuwa mmekuwa nami tangu mwanzo.
\fr 15:25
\f Taz Zab 35:19;69:4

\c 16

1 “Nimewaambieni hayo kusudi msiiache imani yenu.
2 Watu watawatenga ninyi na masunagogi yao. Tena, wakati unakuja
ambapo kila atakayewaua ninyi atadhani anamhudumia Mungu.
3 Watawatendeeni mambo hayo kwa sababu hawamjui Baba, wala hawanijui
mimi.
4 Basi, nimewaambieni mambo haya ili saa yake itakapofika mkumbuke
kwamba niliwaambieni.

Kazi ya Roho Mtakatifu
“Sikuwaambieni mambo haya tangu mwanzo kwa sababu nilikuwa pamoja
nanyi.
5 Lakini sasa namwendea yule aliyenituma; na hakuna hata mmoja wenu
anayeniuliza: <Unakwenda wapi?>
6 Kwa kuwa nimewaambieni mambo hayo mmejaa huzuni mioyoni mwenu.
7 Lakini, nawaambieni ukweli: afadhali kwenu mimi niende zangu,
maana nisipokwenda Msaidizi hatakuja kwenu. Lakini nikienda, basi,
nitamtuma kwenu.
8 Naye atakapokuja atawathibitishia walimwengu kwamba wamekosea
kuhusu dhambi, uadilifu na hukumu ya Mungu.
9 Wamekosea kuhusu dhambi kwa sababu hawaniamini;
10 kuhusu uadilifu, kwa sababu naenda zangu kwa Baba, nanyi
hamtaniona tena;
11 kuhusu hukumu kwa sababu mkuu wa ulimwengu huu amekwisha
hukumiwa.

12 “Ninayo bado mengi ya kuwaambieni, ila kwa sasa hamwezi
kuyastahimili.
13 Lakini atakapokuja huyo Roho wa kweli atawaongoza kwenye ukweli
wote; maana hatasema kwa mamlaka yake mwenyewe, bali atawaambieni yote
atakayosikia, na atasema mambo yatakayokuwa yanakuja.
14 Yeye atanitukuza mimi kwa kuwa atawaambieni yale atakayopata
kutoka kwangu.
15 Vyote alivyo navyo Baba ni vyangu; ndiyo maana nimesema kwamba
huyo Roho Mtakatifu atawaambieni yale atakayopata kutoka kwangu.

Huzuni na furaha

16 “Bado kitambo kidogo nanyi hamtaniona; na baada ya kitambo
kidogo tena mtaniona!”
17 Hapo baadhi ya wanafunzi wake wakaulizana, “Ana maana gani
anapotwambia: <Bado kitambo kidogo nanyi hamtaniona; na baada ya kitambo
kidogo tena mtaniona?> Tena anasema: <Kwa kuwa ninakwenda kwa Baba!”>
18 Basi, wakawa wanaulizana, “Ana maana gani anaposema: <Bado
kitambo kidogo?> Hatuelewi anaongelea nini.”
19 Yesu alijua kwamba walitaka kumwuliza, basi akawaambia, “Je,
mnaulizana juu ya yale niliyosema: <Bado kitambo kidogo nanyi
hamtaniona; na baada ya kitambo kidogo tena mtaniona?>
20 Nawaambieni kweli, ninyi mtalia na kuomboleza, lakini ulimwengu
utafurahi: mtaona huzuni lakini huzuni yenu itageuka kuwa furaha.
21 Wakati mama anapojifungua huona huzuni kwa sababu saa ya maumivu
imefika; lakini akisha jifungua hayakumbuki tena maumivu hayo kwa sababu
ya furaha kwamba mtu amezaliwa duniani.
22 Ninyi pia mna huzuni sasa; lakini nitawajieni tena, nanyi mtajaa
furaha mioyoni mwenu, na furaha hiyo hakuna mtu atakayeiondoa kwenu.
23 Siku hiyo hamtaniomba chochote. Kweli nawaambieni, chochote
mtakachomwomba Baba kwa jina langu, atawapeni.
24 Mpaka sasa hamjaomba chochote kwa jina langu. Ombeni nanyi
mtapata ili furaha yenu ikamilike.

Nimeushinda ulimwengu

25 “Nimewaambieni mambo hayo kwa mafumbo. Lakini wakati utakuja
ambapo sitasema tena nanyi kwa mafumbo, bali nitawaambieni waziwazi juu
ya Baba.
26 Siku hiyo mtaomba kwa jina langu, na siwaambii kwamba nitamwomba
Baba kwa niaba yenu;
27 maana yeye mwenyewe anawapenda ninyi, kwa sababu ninyi mmenipenda
mimi na mmeamini kwamba nimetoka kwa Mungu.
28 Mimi nilitoka kwa Baba, nikaja ulimwenguni; na sasa nauacha
ulimwengu na kurudi kwa Baba.”

29 Basi, wanafunzi wake wakamwambia, “Ahaa! Sasa unasema waziwazi
kabisa bila kutumia mafumbo.
30 Sasa tunajua kwamba wewe unajua kila kitu, na huna haja ya
kuulizwa maswali na mtu yeyote; kwa hiyo tunaamini kwamba umetoka kwa
Mungu.”
31 Yesu akawajibu, “Je, mnaamini sasa?
32 Wakati unakuja, tena umekwisha fika, ambapo ninyi nyote
mtatawanyika kila mtu kwake, nami nitaachwa peke yangu. Kumbe, lakini
mimi siko peke yangu, maana Baba yu pamoja nami.
33 Nimewaambieni mambo haya ili mpate kuwa na amani katika kuungana
nami. Ulimwenguni mtapata masumbuko; lakini jipeni moyo! Mimi
nimeushinda ulimwengu!”

\c 17

Yesu anawaombea wanafunzi wake

1 Yesu alipokwisha sema hayo, alitazama juu mbinguni, akasema,
“Baba, saa imefika! Mtukuze Mwanao ili naye Mwana apate kukutukuza.
2 Maana ulimpa Mwanao mamlaka juu ya watu wote ili awape uzima wa
milele wote hao uliompa.
3 Na uzima wa milele ndio huu: kukujua wewe uliye peke yako Mungu wa
kweli, na kumjua Yesu Kristo uliyemtuma.
4 Mimi nimekutukuza hapa duniani; nimeikamilisha ile kazi uliyonipa
nifanye.
5 Sasa, Baba, nitukuze mbele yako kwa ule utukufu niliokuwa nao
kabla ya kuumbwa ulimwengu.

6 “Nimekufanya ujulikane kwa watu wale ulionipa kutoka duniani.
Walikuwa watu wako, nawe ukanipa wawe wangu; nao wamelishika neno lako.
7 Sasa wanajua kwamba kila ulichonipa kimetoka kwako.
8 Mimi nimewapa ule ujumbe ulionipa nao wameupokea; wanajua kwamba
kweli nimetoka kwako, na wanaamini kwamba wewe ulinituma.

9 “Nawaombea hao; siuombei ulimwengu, ila nawaombea hao ulionipa,
maana ni wako.
10 Yote niliyo nayo ni yako, na yako ni yangu; na utukufu wangu
umeonekana ndani yao.
11 Na sasa naja kwako; simo tena ulimwenguni, lakini wao wamo
ulimwenguni. Baba Mtakatifu! Kwa nguvu ya jina lako ulilonipa, tafadhali
uwaweke salama ili wawe kitu kimoja kama sisi tulivyo mmoja.
12 Nilipokuwa nao, mimi niliwaweka salama kwa nguvu ya jina lako
ulilonipa. Mimi nimewalinda, wala hakuna hata mmoja wao aliyepotea,
isipokuwa yule aliyelazimika kupotea ili Maandiko Matakatifu yapate
kutimia.
13 Basi, sasa naja kwako, na nimesema mambo haya ulimwenguni, ili
waweze kushiriki kikamilifu furaha yangu.
14 Mimi nimewapa neno lako, nao ulimwengu ukawachukia, kwa sababu
wao si wa ulimwengu kama vile nami nisivyo wa ulimwengu.
15 Siombi uwatoe ulimwenguni, bali naomba uwakinge na yule Mwovu.
16 Wao si wa ulimwengu, kama vile nami nisivyo wa ulimwengu.
17 Waweke wakfu kwa ukweli; neno lako ni ukweli.
18 Kama vile ulivyonituma ulimwenguni, nami pia nimewatuma wao
ulimwenguni;
19 na kwa ajili yao mimi mwenyewe najiweka wakfu ili nao pia
wafanywe wakfu katika ukweli.

20 “Siwaombei hao tu, bali nawaombea pia wote watakaoamini kutokana
na ujumbe wao.
21 Naomba ili wote wawe kitu kimoja. Baba! Naomba wawe ndani yetu
kama vile wewe ulivyo ndani yangu nami ndani yako. Naomba wawe kitu
kimoja kusudi ulimwengu upate kuamini kwamba wewe ulinituma.
22 Mimi nimewapa utukufu uleule ulionipa mimi, ili wawe kitu kimoja
kama nasi tulivyo mmoja;
23 mimi niwe ndani yao, nawe uwe ndani yangu; naomba wakamilishwe na
kuwa kitu kimoja, ili ulimwengu upate kujua kwamba wewe ulinituma, na
kwamba unawapenda wao kama unavyonipenda mimi.

24 “Baba! Nataka wao ulionipa wawe pamoja nami pale nilipo, ili
wauone utukufu wangu ulionipa; kwa kuwa ulinipenda kabla ya kuumbwa
ulimwengu.
25 Baba Mwema! Ulimwengu haukujui, lakini mimi nakujua. Hawa nao
wanajua kwamba wewe ulinituma.
26 Nimekufanya ujulikane kwao na nitaendelea kufanya hivyo, ili
upendo ulio nao kwangu uwe ndani yao, nami niwe ndani yao.”

\c 18

Yesu anatiwa nguvuni
\r
\is (Mat. 26:47-57; Marko 14:43-50; Luka 22:47-53)
\ie

1 Yesu alipokwisha sema hayo, alikwenda ng’ambo ya kijito Kedroni,
pamoja na wanafunzi wake. Mahali hapo palikuwa na bustani, naye Yesu
akaingia humo pamoja na wanafunzi wake.
2 Yuda, aliyemsaliti Yesu, alipajua mahali hapo kwani mara nyingi
Yesu alikutana na wanafunzi wake huko.
3 Basi, Yuda alichukua kikosi cha askari na walinzi kutoka kwa
makuhani wakuu na Mafarisayo, akaja nao bustanini wakiwa na taa, mienge
na silaha.
4 Yesu, hali akijua yote yatakayompata, akatokea, akawauliza,
“Mnamtafuta nani?”
5 Nao wakamjibu, “Yesu wa Nazareti!” Yesu akawaambia, “Mimi
ndiye.” Msaliti Yuda alikuwa amesimama hapo pamoja nao.

6 Basi, Yesu alipowaambia: “Mimi ndiye”, wakarudi nyuma,
wakaanguka chini.
7 Yesu akawauliza tena, “Mnamtafuta nani?” Wakamjibu, “Yesu wa
Nazareti!”
8 Yesu akawaambia, “Nimekwisha waambieni kwamba mimi ndiye. Basi,
kama mnanitafuta mimi, waacheni hawa waende zao.” (((
9 Alisema hayo ili yapate kutimia yale aliyosema: “Wale ulionipa
sikumpoteza hata mmoja.”)
10 Simoni Petro alikuwa na upanga; basi, akauchomoa, akamkata sikio
la kulia mtumishi wa Kuhani Mkuu. Mtumishi huyo aliitwa Malko.
11 Basi, Yesu akamwambia Petro, “Rudisha upanga wako alani. Je,
nisinywe kikombe alichonipa Baba?”

Yesu mbele ya Kuhani Mkuu

12 Kile kikosi cha askari, mkuu wake na walinzi wa Wayahudi
walimkamata Yesu, wakamfunga
13 na kumpeleka kwanza kwa Anasi; Anasi alikuwa baba mkwe wa Kayafa
ambaye alikuwa Kuhani Mkuu mwaka huo.
14 Huyo Kayafa ndiye aliyekuwa amewashauri Wayahudi kwamba ni
afadhali mtu mmoja afe kwa ajili ya taifa.

Petro anamkana Yesu
\r
\is (Mat. 26:69-70; Marko 14:66-68; Luka 22:55-57)
\ie

15 Simoni Petro pamoja na mwanafunzi mwingine walimfuata Yesu. Huyo
mwanafunzi mwingine alikuwa anajulikana kwa Kuhani Mkuu, hivyo aliingia
pamoja na Yesu ndani ya ukumbi wa Kuhani Mkuu.
16 Lakini Petro alikuwa amesimama nje, karibu na mlango. Basi, huyo
mwanafunzi mwingine aliyekuwa anajulikana kwa Kuhani Mkuu alitoka nje
akasema na mjakazi, mngoja mlango, akamwingiza Petro ndani.
17 Huyo msichana mngoja mlango akamwuliza Petro, “Je, nawe pia ni
mmoja wa wanafunzi wa mtu huyu?” Petro akamwambia, “Si mimi!”

18 Watumishi na walinzi walikuwa wamewasha moto kwa sababu kulikuwa
na baridi, wakawa wanaota moto. Naye Petro alikuwa amesimama pamoja nao
akiota moto.

Kuhani Mkuu anamhoji Yesu
\r
\is (Mat. 26:59-66; Marko 14:55-64; Luka 22:66-71)
\ie

19 Basi, Kuhani akamwuliza Yesu juu ya wanafunzi wake na mafundisho
yake.
20 Yesu akamjibu, “Nimesema na kila mtu daima hadharani. Kila mara
nimefundisha katika masunagogi na Hekaluni, mahali wakutanikiapo
Wayahudi wote; na wala sijasema chochote kwa siri.
21 Kwa nini waniuliza mimi? Waulize wale waliosikia nini
niliwaambia. Wao wanajua nilivyosema.”
22 Alipokwisha sema hayo mlinzi mmoja aliyekuwa amesimama hapo
akampiga kofi akisema, “Je, ndivyo unavyomjibu Kuhani Mkuu?”
23 Yesu akamjibu, “Kama nimesema vibaya, onyesha huo ubaya; lakini
ikiwa nimesema vema, mbona wanipiga?”
24 Basi, Anasi akampeleka Yesu akiwa amefungwa, kwa Kuhani Mkuu
Kayafa.

Petro anamkana Yesu tena
\r
\is (Mat. 26:71-75; Marko 14:69-72; Luka 22:58-62)
\ie

25 Petro alikuwa hapo akiota moto. Basi, wakamwuliza, “Je, nawe pia
si mmoja wa wanafunzi wake?” Yeye akakana na kusema, “Si mimi!”
26 Mmoja wa watumishi wa Kuhani Mkuu, jamaa wa yule aliyekatwa sikio
na Petro, akamwuliza, “Je, mimi sikukuona wewe bustanini pamoja naye?”
27 Petro akakana tena; mara jogoo akawika.

Yesu mbele ya Pilato
\r
\is (Mat. 27:1-2, 11-14; Marko 15:1-5; Luka 23:1-5)
\ie

28 Basi, walimchukua Yesu kutoka kwa Kayafa, wakampeleka ikulu.
Ilikuwa alfajiri, nao ili waweze kula Pasaka, hawakuingia ndani ya ikulu
wasije wakatiwa najisi.
29 Kwa hiyo, Pilato aliwaendea nje, akasema, “Mna mashtaka gani juu
ya mtu huyu?”
30 Wakamjibu, “Kama huyu hangalikuwa mwovu hatungalimleta kwako.”
31 Pilato akawaambia, “Haya, mchukueni ninyi wenyewe, mkamhukumu
kufuatana na Sheria yenu.” Wayahudi wakamjibu, “Sisi hatuna mamlaka ya
kumwua mtu yeyote.” (((
32 Ilifanyika hivyo yapate kutimia maneno aliyosema Yesu kuonyesha
atakufa kifo gani.)
33 Pilato akaingia tena ndani ya ikulu, akamwita Yesu na kumwuliza:
“Ati wewe ndiye Mfalme wa Wayahudi?”
34 Yesu akamjibu, “Je, hayo ni maneno yako au wengine wamekwambia
habari zangu?”
35 Pilato akamjibu, “Je, ni Myahudi mimi? Taifa lako na makuhani
wamekuleta kwangu. Umefanya nini?”
36 Yesu akamjibu, “Ufalme wangu si wa ulimwengu huu. Kama ufalme
wangu ungekuwa wa ulimwengu huu watumishi wangu wangenipigania nisitiwe
mikononi mwa Wayahudi. Lakini sasa ufalme wangu si wa hapa.”
37 Hapo Pilato akamwambia, “Basi, wewe ni Mfalme?” Yesu akajibu,
“Wewe umesema kwamba mimi ni Mfalme. Mimi nimezaliwa kwa ajili hiyo; na
kwa ajili hiyo nimekuja ulimwenguni kuwaambia watu juu ya ukweli. Kila
mtu wa ukweli hunisikiliza.”
38 Pilato akamwambia, “Ukweli ni kitu gani?”

Yesu anahukumiwa kufa
\r
\is (Mat. 27:15-31; Marko 15:6-20; Luka 23:13-25)
\ie
Pilato alipokwisha sema hayo, aliwaendea tena Wayahudi nje,
akawaambia, “Mimi sioni hatia yoyote kwake.
39 Lakini, mnayo desturi kwamba mimi niwafungulie mfungwa mmoja
wakati wa Pasaka. Basi, mwataka niwafungulieni Mfalme wa Wayahudi?”
40 Hapo wakapiga kelele: “La! Si huyu ila Baraba!” Naye Baraba
alikuwa mnyang’anyi.

\c 19

1 Basi, Pilato akaamuru Yesu achukuliwe, apigwe viboko.
2 Nao askari wakasokota taji ya miiba, wakamtia kichwani, wakamvika
na joho la rangi ya zambarau.
3 Wakawa wanakuja mbele yake na kusema: “Shikamoo, Mfalme wa
Wayahudi!” Wakampiga makofi.
4 Pilato akatoka tena nje, akawaambia, “Tazameni, namleta nje
kwenu, mpate kujua kwamba mimi sikuona hatia yoyote kwake.”
5 Basi, Yesu akatoka nje amevaa taji ya miiba na joho la rangi ya
zambarau. Pilato akawaambia, “Tazameni! Mtu mwenyewe ni huyo.”
6 Makuhani wakuu na walinzi walipomwona wakapaaza sauti:
“Msulubishe! Msulubishe!” Pilato akawaambia, “Mchukueni basi, ninyi
wenyewe mkamsulubishe, kwa maana mimi sikuona hatia yoyote kwake.”
7 Wayahudi wakamjibu, “Sisi tunayo Sheria, na kufuatana na Sheria
hiyo, ni lazima afe, kwa sababu alijifanya kuwa Mwana wa Mungu.”

8 Pilato aliposikia maneno hayo akazidi kuogopa.
9 Basi, akaingia tena ndani ya ikulu, akamwuliza Yesu, “Umetoka
wapi wewe?” Lakini Yesu hakumjibu neno.
10 Hivyo Pilato akamwambia, “Husemi nami? Je, hujui kwamba ninayo
mamlaka ya kukufungua na mamlaka ya kukusulubisha?”
11 Yesu akamjibu, “Hungekuwa na mamlaka yoyote juu yangu kama
hungepewa na Mungu. Kwa sababu hiyo, yule aliyenikabidhi kwako ana
dhambi kubwa zaidi.”
12 Tangu hapo, Pilato akawa anatafuta njia ya kumwachilia, lakini
Wayahudi wakapiga kelele: “Ukimwachilia huyu mtu, wewe si rafiki yake
Kaisari; kila mtu anayejifanya kuwa Mfalme humpinga Kaisari!”
13 Basi, Pilato aliposikia maneno hayo akamleta Yesu nje, akaketi
juu ya kiti cha hukumu, mahali paitwapo: “Sakafu ya Mawe” (kwa
Kiebrania, Gabatha).

14 Ilikuwa yapata saa sita mchana, siku ya maandalio ya Pasaka.
Pilato akawaambia Wayahudi, “Tazameni, Mfalme wenu!”
15 Wao wakapaaza sauti: “Mwondoe! Mwondoe! Msulubishe!” Makuhani
wakuu wakajibu, “Sisi hatuna Mfalme isipokuwa Kaisari!”
16 Basi, hapo Pilato akamtia Yesu mikononi mwao ili asulubiwe.

Yesu anasulubiwa msalabani
\r
\is (Mat. 27:32-44; Marko 15:21-32; Luka 23:26-43)
\ie
Basi, wakamchukua Yesu.
17 Naye akatoka akiwa amejichukulia msalaba wake kwenda mahali
paitwapo “Fuvu la Kichwa”, (kwa Kiebrania Golgotha).
18 Hapo ndipo walipomsulubisha, na pamoja naye waliwasulubisha watu
wengine wawili; mmoja upande wake wa kulia na mwingine upande wake wa
kushoto, naye Yesu katikati.
19 Pilato aliandika ilani akaiweka juu ya msalaba. Nayo ilikuwa
imeandikwa hivi: “Yesu wa Nazareti, Mfalme wa Wayahudi.”
20 Wayahudi wengi waliisoma ilani hiyo, maana mahali hapo
aliposulubiwa Yesu palikuwa karibu na mji. Tena ilani hiyo ilikuwa
imeandikwa kwa Kiebrania, Kilatini, na Kigiriki.
21 Basi, makuhani wakuu wakamwambia Pilato, “Usiandike: <Mfalme wa
Wayahudi>, ila <Yeye alisema, Mimi ni Mfalme wa Wayahudi.”>
22 Pilato akajibu, “Niliyoandika, nimeandika!”

23 Askari walipokwisha msulubisha Yesu, walizichukua nguo zake,
wakazigawa mafungu manne, fungu moja kwa kila askari. Walichukua pia na
kanzu yake; kanzu hiyo ilikuwa imefumwa kwa kipande kimoja tu, bila
mshono.
24 Basi, hao askari wakashauriana: “Tusiipasue, ila tuipigie kura
itakuwa ya nani.” Jambo hilo lilifanyika ili yatimie Maandiko
Matakatifu yasemayo:

“Waligawana mavazi yangu,
na nguo yangu wakaipigia kura.”
\m Basi, ndivyo walivyofanya hao askari.
\il 5
ic
\is Askari waroma (Yoh 19:23)
\ie

25 Karibu na msalaba wake Yesu walikuwa wamesimama mama yake, na
dada ya mama yake, Maria mke wa Kleopa, na Maria Magdalene.
26 Yesu alipomwona mama yake, na karibu naye amesimama yule
mwanafunzi aliyempenda, akamwambia mama yake: “Mama! Tazama, huyo ndiye
mwanao.”
27 Halafu akamwambia yule mwanafunzi: “Tazama, huyo ndiye mama
yako.” Na tangu saa ile huyo mwanafunzi alimchukua akae nyumbani kwake.
\fr 19:24
\f Taz Zab 22:18

Yesu anakufa
\r
\is (Mat. 27:45-56; Marko 15:33-41; Luka 23:44-49)
\ie

28 Yesu alijua kwamba yote yalikuwa yametimia; na, ili Maandiko
Matakatifu yapate kutimia, akasema, “Naona kiu.”
29 Hapo palikuwa na bakuli limejaa siki. Basi, wakachovya sifongo
katika hiyo siki, wakaitia juu ya ufito wa husopo, wakamwekea mdomoni.
30 Yesu alipokwisha pokea hiyo siki, akasema, “Yametimia!” Kisha
akainama kichwa, akatoa roho.
\fr 19:28
\f Taz Zab 22:15; 69:21

Yesu anachomwa mkuki ubavuni

31 Ilikuwa Ijumaa, siku ya Maandalio. Kwa hiyo, kusudi miili isikae
msalabani siku ya Sabato, maana siku hiyo ya Sabato ilikuwa siku kubwa,
Wayahudi walimwomba Pilato miguu ya hao waliosulubiwa ivunjwe na miili
yao iondolewe.
32 Basi, askari walikwenda, wakaivunja miguu ya yule mtu wa kwanza
na yule wa pili ambao walikuwa wamesulubiwa pamoja na Yesu.
33 Lakini walipomfikia Yesu waliona kwamba alikwisha kufa, na hivyo
hawakumvunja miguu.
34 Lakini askari mmoja alimtoboa ubavuni kwa mkuki, na mara ikatoka
damu na maji. (((
35 Naye aliyeona tukio hilo ametoa habari zake ili nanyi mpate
kuamini. Na hayo aliyosema ni ukweli, tena yeye anajua kwamba anasema
ukweli.)
36 Jambo hilo lilitendwa ili Maandiko Matakatifu yatimie: “Hapana
hata mfupa wake mmoja utakaovunjwa.”
37 Tena Maandiko mengine yanasema: “Watamtazama yule
waliyemtoboa.”
\fr 19:36
\f Taz Zab 34:20

Yesu anazikwa kaburini
\r
\is (Mat. 27:57-61; Marko 15:42-47; Luka 23:50-56)
\ie

38 Baada ya hayo, Yosefu, mwenyeji wa Armathaya, alimwomba Pilato
ruhusa ya kuuchukua mwili wa Yesu. (Yosefu alikuwa mfuasi wa Yesu,
lakini kwa siri, maana aliwaogopa viongozi wa Wayahudi). Basi, Pilato
akamruhusu. Hivyo Yosefu alikwenda, akauondoa mwili wa Yesu.
39 Naye Nikodemo ambaye hapo awali alikuwa amemwendea Yesu usiku,
akaja akiwa amechukua mchanganyiko wa manemane na ubani kiasi cha kilo
thelathini.
40 Basi, waliutwaa mwili wa Yesu, wakaufunga sanda pamoja na
manukato kufuatana na desturi ya Wayahudi katika kuzika.
41 Mahali hapo aliposulubiwa Yesu palikuwa na bustani, na katika
bustani hiyo kulikuwa na kaburi jipya ambalo hakutiwa bado mtu yeyote
ndani yake.
42 Basi, kwa sababu ya shughuli za Wayahudi za maandalio ya Sabato,
na kwa vile kaburi hilo lilikuwa karibu, wakamweka Yesu humo.

\c 20

Kaburi tupu
\r
\is (Mat. 28:1-8; Marko 16:1-8; Luka 24:1-12)
\ie

1 Alfajiri na mapema Jumapili, kukiwa bado na giza, Maria Magdalene
alikwenda kaburini, akaliona lile jiwe limeondolewa mlangoni pa kaburi.
2 Basi, akaenda mbio hadi kwa Petro na yule mwanafunzi mwingine
ambaye Yesu alimpenda, akawaambia, “Wamemwondoa Bwana kaburini, na wala
hatujui walikomweka.”
3 Petro pamoja na yule mwanafunzi mwingine wakaenda kaburini.
4 Wote wawili walikimbia lakini yule mwanafunzi mwingine alikimbia
mbio zaidi kuliko Petro, akatangulia kufika kaburini.
5 Alipoinama na kuchungulia ndani, aliona sanda, lakini hakuingia
ndani.
6 Simoni Petro naye akaja akimfuata, akaingia kaburini; humo akaona
sanda,
7 na kile kitambaa alichofungwa Yesu kichwani. Hicho kitambaa
hakikuwekwa pamoja na hiyo sanda, bali kilikuwa kimekunjwa na kuwekwa
mahali peke yake.
8 Kisha yule mwanafunzi mwingine aliyemtangulia kufika kaburini,
akaingia pia ndani, akaona, akaaamini. (((
9 Walikuwa bado hawajaelewa Maandiko Matakatifu yaliyosema kwamba
ilikuwa lazima afufuke kutoka wafu).
10 Basi, hao wanafunzi wakarudi nyumbani.

Yesu anamtokea Maria Magdalene
\r
\is (Mat. 28:9-10; Marko 16:9-11)
\ie

11 Maria alikuwa amesimama nje ya kaburi, akilia. Huku akiwa bado
analia, aliinama na kuchungulia kaburini,
12 akawaona malaika wawili waliovaa mavazi meupe, wameketi pale
mwili wa Yesu ulipokuwa umelazwa, mmoja kichwani na wa pili miguuni.
13 Hao malaika wakamwuliza, “Mama, kwa nini unalia?” Naye
akawaambia, “Wamemwondoa Bwana wangu, na wala sijui walikomweka!”

14 Baada ya kusema hayo, aligeuka nyuma, akamwona Yesu amesimama
hapo, lakini asitambue ya kuwa ni Yesu.
15 Yesu akamwuliza, “Mama, kwa nini unalia? Unamtafuta nani?”
Maria, akidhani kwamba huyo ni mtunza bustani, akamwambia, “Mheshimiwa,
kama ni wewe umemwondoa, niambie ulikomweka, nami nitamchukua.”
16 Yesu akamwambia, “Maria!” Naye Maria akageuka, akamwambia kwa
Kiebrania, “Raboni” (yaani “Mwalimu”).
17 Yesu akamwambia, “Usinishike; sijakwenda bado juu kwa Baba.
Lakini nenda kwa ndugu zangu uwaambie: nakwenda juu kwa Baba yangu na
Baba yenu, Mungu wangu na Mungu wenu.”
18 Hivyo Maria Magdalene akaenda akawapa habari wale wanafunzi kuwa
amemwona Bwana, na kwamba alikuwa amemwambia hivyo.

Yesu anawatokea wanafunzi wake
\r
\is (Mat. 28:16-20; Marko 16:14-18; Luka 24:36-49)
\ie

19 Ilikuwa jioni ya siku hiyo ya Jumapili. Wanafunzi walikuwa
wamekutana pamoja ndani ya nyumba, na milango ilikuwa imefungwa kwa
sababu waliwaogopa viongozi wa Wayahudi. Basi, Yesu akaja, akasimama
kati yao, akawaambia, “Amani kwenu!”
20 Alipokwisha sema hayo, akawaonyesha mikono yake na ubavu wake.
Basi, hao wanafunzi wakafurahi mno kumwona Bwana.
21 Yesu akawaambia tena, “Amani kwenu! Kama vile Baba alivyonituma
mimi, nami nawatuma ninyi.”
22 Alipokwisha sema hayo, akawapulizia na kuwaambia, “Pokeeni Roho
Mtakatifu.
23 Mkiwasamehe watu dhambi zao, wamesamehewa; msipowaondolea,
hawasamehewi.”

Yesu na Thoma

24 Thoma mmoja wa wale kumi na wawili (aitwaye Pacha), hakuwa pamoja
nao wakati Yesu alipokuja.
25 Basi, wale wanafunzi wengine wakamwambia, “Tumemwona Bwana.”
Thoma akawaambia, “Nisipoona mikononi mwake alama za misumari, na kutia
kidole changu katika kovu hizo, na kutia mkono wangu ubavuni mwake,
sitasadiki.”

26 Basi, baada ya siku nane hao wanafunzi walikuwa tena pamoja mle
ndani, na Thoma alikuwa pamoja nao. Milango ilikuwa imefungwa, lakini
Yesu akaja, akasimama kati yao, akasema, “Amani kwenu!”
27 Kisha akamwambia Thoma, “Lete kidole chako hapa uitazame mikono
yangu; lete mkono wako ukautie ubavuni mwangu. Usiwe na mashaka, ila
amini!”
28 Thoma akamjibu, “Bwana wangu na Mungu wangu!”
29 Yesu akamwambia, “Je, unaamini kwa kuwa umeniona? Heri yao wale
ambao hawajaona, lakini wameamini.”

Shabaha ya kitabu

30 Yesu alifanya mbele ya wanafunzi wake ishara nyingine nyingi
ambazo hazikuandikwa katika kitabu hiki.
31 Lakini hizi zimeandikwa ili mpate kuamini kwamba Yesu ni Kristo,
Mwana wa Mungu; na kwa kuamini mpate kuwa na uzima kwa nguvu ya jina
lake.

\c 21

Yesu anawatokea wanafunzi saba

1 Baada ya hayo Yesu aliwatokea tena wanafunzi wake kando ya ziwa
Tiberia. Aliwatokea hivi:
2 Simoni Petro, Thoma (aitwaye Pacha), na Nathanieli mwenyeji wa
Kana Galilaya, wana wawili wa Zebedayo na wanafunzi wake wengine wawili,
walikuwa wote pamoja.
3 Simoni Petro aliwaambia, “Nakwenda kuvua samaki.” Nao
wakamwambia, “Nasi tutafuatana nawe.” Basi, wakaenda, wakapanda
mashua, lakini usiku huo hawakupata chochote.
4 Kulipoanza kupambazuka, Yesu alisimama kando ya ziwa, lakini
wanafunzi hawakujua kwamba alikuwa yeye.
5 Basi, Yesu akawauliza, “Vijana, hamjapata samaki wowote sio?”
Wao wakamjibu, “La! Hatujapata kitu.”
6 Yesu akawaambia, “Tupeni wavu upande wa kulia wa mashua nanyi
mtapata samaki.” Basi, wakatupa wavu lakini sasa hawakuweza kuuvuta
tena kwa wingi wa samaki.
7 Hapo yule mwanafunzi aliyependwa na Yesu akamwambia Petro, “Ni
Bwana!” Simoni Petro aliposikia ya kuwa ni Bwana, akajifunga vazi lake
(maana hakuwa amelivaa), akarukia majini.
8 Lakini wale wanafunzi wengine walikuja pwani kwa mashua huku
wanauvuta wavu uliojaa samaki; hawakuwa mbali na nchi kavu, ila walikuwa
yapata mita mia moja kutoka ukingoni.
9 Walipofika nchi kavu waliona moto wa makaa umewashwa na juu yake
pamewekwa samaki na mkate.
10 Yesu akawaambia, “Leteni hapa baadhi ya samaki mliovua.”
11 Basi, Simoni Petro akapanda mashuani, akavuta hadi nchi kavu ule
wavu uliokuwa umejaa samaki wakubwa mia moja na hamsini na watatu. Na
ingawa walikuwa wengi hivyo wavu haukukatika.
12 Yesu akawaambia, “Njoni mkafungue kinywa.” Hakuna hata mmoja
wao aliyethubutu kumwuliza: “Wewe ni nani?” Maana walijua alikuwa
Bwana.
13 Yesu akaja, akatwaa mkate akawapa; akafanya vivyo hivyo na wale
samaki.

14 Hii ilikuwa mara ya tatu Yesu kuwatokea wanafunzi wake baada ya
kufufuka kutoka wafu.

Yesu na Petro

15 Walipokwisha kula, Yesu alimwuliza Simoni Petro, “Simoni, mwana
wa Yohane! Je, wanipenda mimi zaidi kuliko hawa?” Naye akajibu, “Naam,
Bwana; wajua kwamba mimi nakupenda.” Yesu akamwambia, “Tunza wana
kondoo wangu.”

16 Kisha akamwambia mara ya pili, “Simoni mwana wa Yohane! Je,
wanipenda?” Petro akamjibu, “Naam, Bwana; wajua kwamba nakupenda.”
Yesu akamwambia, “Tunza kondoo wangu.”

17 Akamwuliza mara ya tatu, “Simoni mwana wa Yohane! Je,
wanipenda?” Hapo Petro akahuzunika kwa sababu alimwuliza mara ya tatu:
“Wanipenda?” akamwambia, “Bwana, wewe wajua yote; wewe wajua kwamba
mimi nakupenda.” Yesu akamwambia, “Tunza kondoo wangu!
18 Kweli nakwambia, ulipokuwa kijana ulizoea kujifunga mshipi na
kwenda kokote ulikotaka. Lakini utakapokuwa mzee utanyosha mikono yako,
na mtu mwingine atakufunga na kukupeleka usikopenda kwenda.”
19 (Kwa kusema hivyo, alionyesha jinsi Petro atakavyokufa na
kumtukuza Mungu.) Kisha akamwambia, “Nifuate.”

Yesu na yule mwanafunzi mwingine

20 Hapo Petro akageuka, akamwona yule mwanafunzi ambaye Yesu
alimpenda, anafuata (Huyu mwanafunzi ndiye yule ambaye wakati wa chakula
cha jioni, alikaa karibu sana na Yesu na kumwuliza: “Bwana ni nani
atakayekusaliti?”)
21 Basi, Petro alipomwona huyo akamwuliza Yesu, “Bwana, na huyu
je?”
22 Yesu akamjibu, “Kama nataka abaki mpaka nitakapokuja, yakuhusu
nini? Wewe nifuate mimi.”
23 Basi, habari hiyo ikaenea miongoni mwa wale ndugu kwamba
mwanafunzi huyo hafi. Lakini Yesu hakumwambia kwamba mwanafunzi huyo
hafi, ila, “Kama nataka abaki mpaka nitakapokuja, yakuhusu nini?”

24 Huyo ndiye yule aliyeshuhudia mambo haya na kuyaandika. Nasi
twajua kwamba aliyoyasema ni kweli.

Hatima

25 Kuna mambo mengine mengi aliyofanya Yesu, ambayo kama
yangeandikwa yote, moja baada ya lingine, nadhani hata ulimwengu wenyewe
usingetosha kuviweka vitabu ambavyo vingeandikwa.